Serikali yasikitishwa Denmark kufunga ubalozi wake Tanzania

August 28, 2021 12:29 pm · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Yasema Serikali imefanya juhudi kubwa za kufufua na kuimarisha diplomasia ya kimataifa.
  • Yasema inaamini nchi hiyo itaendelea kushirikiana na Tanzania.
  • Denmark yasema Tanzania imepiga hatua nzuri ya maendeleo hivyo inaenda kuzisaidia nchi nyingine.

Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesikitishwa na hatua ya nchi ya Denmark kuamua kufunga shughuli za ubalozi wake nchini ifikapo mwaka 2024 licha ya jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali za kufufua na kuimarisha diplomasia na uhusiano wa kimataifa.

Denmark iliyokuwepo nchini kwa takribani miongo sita, imetangaza kuufunga ubalozi wake nchini Tanzania kwa sababu inataka kuendana na mpango wa nchi hiyo katika masuala ya kimataifa.

Uamuzi huo ulitangazwa jana Agosti 27, 2021) na Waziri wa Mambo ya nje wa Denmark, Jeppe Kofod ambapo amesema ni matokeo ya sehemu ya marekebisho ya Denmark ya uwepo wake kimataifa. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula amesema uamuzi huo wa Demark umekuja wakati  Serikali inayoongozwa Rais Samia Suluhu Hassan imefanya jitihada kubwa za kufufua na kuimarisha diplomasia na uhusiano wa nchi rafiki ikiwemo Denmark.

Balozi Mulamula amesema pia Serikali imeimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji pamoja na kuimarisha demokrasia na utawala wa sheria.

“Pamoja na hatua hiyo iliyochukuliwa na Denmark, ni matarajio ya Tanzania kuwa Serikali ya Denmark itaendelea kushirikiana na Tanzania kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kuunga mkono ajenda za Tanzania katika Umoja wa Ulaya, Umoja wa Mataifa na majukwaa mengine ya kimataifa,” amesema waziri huyo katika taarifa yake iliyotolewa leo Agosti 28, 2021.


TANGAZO


Mulamula ametoa kauli hiyo jana nchini Marekani alipokuwa anazungumza kwa njia ya mtandao na Waziri wa Ushirikiano na Maendeleo wa Denmark, Flemming Mortensen.

Mortensen amesema haikua rahisi kufikia uamuzi huo ambao umezingatia vipaumbele vipya vya Serikali ya Denmark katika ushirikiano wake wa maendeleo vilivyoainishwa katika mkakati wake uitwao “The World We Share”.

Waziri huyo amesema kutokana na Tanzania kufikia hatua nzuri ya maendeleo, nchi yake imeamua kufanya kazi kwa karibu na nchi zenye machafuko na migogoro zikiwemo za Pembe ya Afrika na kuwa hatua hiyo haimaanishi kuwa urafiki kati ya nchi hizo mbili unakufa.  

Mbali na Tanzania, nchi hiyo pia itafunga ubalozi wake nchini Argentina, Ubalozi mdogo wa Chongqing nchini China na ujumbe wa biashara huko Barcelona (Uhispania) na inaelezwa kuwa jumla ya uwakilishi 16 na ofisi tisa katika makao makuu ya Wizara ya Mambo ya Nje huko Copenhagen zitaimarishwa.

Aidha, Denmark imesema itaheshimu ahadi zilizokubaliwa za kifedha na shughuli ya kufunga ubalozi imetengewa fungu ili kuhakikisha mchakato huo unakamilika vizuri.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW