Sikukuu zashusha thamani ya mauzo soko la hisa Dar

Nuzulack Dausen 0250Hrs   Januari 04, 2020 Biashara
  • Kampuni ya bia ya TBL yachangia zaidi ya robo tatu ya thamani ya mauzo hayo

Dar es Salaam. Thamani ya mauzo katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) imeshuka kwa zaidi ya mara nne katika wiki iliyoishia Januari 3, ikichochewa zaidi na sikukuu za mwisho wa mwaka.

Taarifa ya mwenendo wa soko kwa wiki iliyotolewa na kampuni ya udalali ya Zan Securities imesema kuwa thamani ya mauzo ya soko hilo katika wiki ya Desemba 30, 2019 hadi Januari 3, yalikuwa ni Sh418.1 milioni kutoka Sh1.81 bilioni iliyorekodiwa juma lililopita.

“Hali hiyo imechangiwa kwa kiasi kikubwa na sikukuu za mwisho wa mwaka,” inasema taarifa hiyo iliyotolewa na Mtendaji Mkuu wa Zan Securities, Raphael Masumbuko.

Mara nyingi wakati wa sikukuu za mwisho wa mwaka shughuli za kibiashara huwa ni hushuka kidogo kwa kuwa kampuni na wafanyabiashara wengi huwa likizo. 


Zinazohusiana: 


Katika taarifa hiyo, Masumbuko amesema kuwa Kampuni ya bia Tanzania (TBL) ndiyo ilikuwa kinara katika mauzo hayo baada ya kuchangia asilimia 87.8 ya thamani ya mauzo yote ya wiki hiyo.

“Hakuna kaunta iliyorekodi mabadiliko yeyote ya bei,” amesema Masumbuko.

Kwa jumla, Masumbuko amesema mtaji wa soko zima uliongezeka kiduchu kwa asilimia 0.37 hadi Sh17.1 trilioni huku mtaji wa soko la ndani (domestic market capitalisation) ukibaki tambalale wa Sh9 trilioni.

Related Post