Rais Samia kufanya ziara ya siku tano China
- Kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano Kati ya China na Afrika (FOCAC).
- Rais Samia kuomba fedha za miradi minne ya maendeleo.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi ya siku tano nchini China pamoja na kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano Kati ya China na Afrika (Forum on China-Africa Cooperation FOCAC) utakaofanyika jijini Beijing.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu leo Septemba 2, 2024 ziara ya Rais Samia itaanza leo na kutamatika Septemba 6, 2024 ambapo wakati wa ziara hiyo Rais Samia atakutana na Rais wa China, Xi Jinping kwa mazungumzo yanayolenga kuimarisha uhusiano wa kihistoria kati ya mataifa hayo mawili ulioasisiwa miaka 60 iliyopita.
Miongoni mwa maeneo yanayotarajiwa kupewa kipaumbele kwenye Mkutano wa FOCAC ni uendelezaji wa miundombinu, kukuza uwekezaji, uendelezaji wa viwanda, kilimo cha kisasa na amani na usalama.
Rais Samia anatarajia kuwa miongoni mwa Wakuu wa Nchi watakaohutubia ufunguzi wa Mkutano wa FOCAC akizungumza kwa niaba ya Kanda ya Afrika Mashariki.
Pembezoni mwa mkutano huo, katika kukuza biashara na uwekezaji, Rais Samia atakutana na makampuni na wawekezaji kutoka Jamhuri ya Watu wa China kwa lengo la kuhamasisha uwekezaji zaidi nchini Tanzania.
Katika ziara hiyo Rais Samia, Rais wa China Xi Jinping pamoja na Rais wa Zambia Hakainde Hichilema watashiriki na kushuhudia uwekaji saini wa hati za makubaliano ya uboreshaji wa reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA).
Aidha, ziara hiyo imelenga kufanya uboreshaji wa miundombinu kukuza uwekezaji, uendelezaji wa viwanda, kilimo cha kisasa na amani na usalama wa nchi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Agosti 31, 2024 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo alipozungumza na wanahabari, alisema Rais Samia ataenda China kusaka fedha za miradi minne.
“Tanzania inatarajia kuwasilisha miradi mbalimbali ikiwemo mipya na ile ambayo haikuweza kutekelezwa kwenye mpango uliopita wa FOCAC kwa sababu mbalimbali, ili iweze kupatiwa fedha za mkopo nafuu na msaada na kutekelezwa chini ya mpango kazi wa FOCAC mwaka 2025-2027,” alisema Balozi Kombo.
Miradi minne itakayowasilishwa na Rais Samia kwenye mkutano huo ni ujenzi wa mtandao wa mawasiliano vijijini awamu ya pili, ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovoti 400 awamu ya pili na ya tatu, ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi (Veta) awamu ya pili na ujenzi wa barabara za Zanzibar zenye urefu wa kilomita 277.
Hii ni mara ya pili kwa Rais Samia kufanya ziara nchini China katika kipindi cha miaka mitatu ya awamu yake ambapo kwa mara ya kwanza alifanya ziara nchini humo Novemba 02 hadi 04 mwaka 2022.
Latest