Rais Samia: KKK kuimarisha elimu msingi Tanzania
- Mpango huo unatarajiwa kupounga idadi ya wasiojua kusoma kuhesabu na kuandika kufikkia darasa la pili.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imezindua rasmi Mpango Mkakati wa Kisayansi wa Kuimarisha Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK), unaotajwa kuchangia kuimarika kwa elimu msingi nchini.
Rais Samia Suluhu Hassan aliyekuwa akizungumza katika uzinduzi wa mpango huo leo Januari 29,2026 ameeleza kuwa mpango wa KKK ni msingi wa mageuzi ya elimu nchini na ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“KKK ni msingi wa elimu bora na maendeleo ya Taifa. Tunataka kila mtoto aanze safari ya elimu akiwa na umahiri kamili,” amesema Rais Samia.
Mpango wa KKK uliozinduliwa leo unawalenga watoto wa elimu ya awali, darasa la kwanza na darasa la pili, ambao watajifunza kusoma, kuandika na kuhesabu hatua itayowatengenezea msingi imara katua za elimu zinazowasubiri mbeleni.
Naye Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta) Prof Said Mohamedi amesema KKK ni muhimu kama maziwa yalivyo muhimu kwa mtoto mchanga.
“ Kama ambavyo mtoto aliyekosa maziwa ya mama hukosa msingi wa afya, ndivyo pia mtoto aliyekosa umahiri wa KKK hukosa msingi wa elimu,” amesema Profesa Mohamed.
Profesa Mohamed amesema kuwa Necta imekuwa ikifanya upimaji wa umahiri wa KKK kwa njia ya sampuli tangu mwaka 2015, ambapo shule mbili hadi tano zilichaguliwa katika kila halmashauri nchini.
Kwa mujibu wa takwimu za upimaji huo uliohusisha wanafunzi wa darasa la pili na walimu kuanzia 2015 hadi 2023, wanafunzi kati ya asilimia 67 hadi 87 walionyesha umahiri wa kumudu stadi za KKK, idadi inayoendelea kuongezeka kadri watoto wanavyopanda madarasa.
Ili kuhakikisha mpango huo unafanikiwa Rais Samia amemwagiza Waziri wa Elimu Prof Adolf Mkenda pamoja na viongozi wengine wa sekta hiyo kusimamia utekelezaji wa mpango huo usiishie katika makaratasi.
Latest