Rais Samia apiga marufuku uuzwaji holela wa mazao, azitaka Wizara kuandaa mfumo maalum
- Mfumo huo utaiwezesha Serikali kukusanya fedha na kudhibiti wafanyabiashara wasio waaminifu.
- Asema utawaisaidia wakulima kupata faida.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amepiga marufuku uuzwaji holela wa mazao yanayozalishwa nchini unaofanywa na wakulima na kuagiza wizara zinazohusika kuandaa mfumo maalum utakaosimamia mauzo ya mazao nje ya nchi.
Wizara hizo ni pamoja na Wizara ya Kilimo iliyopo chini ya Hussein Bashe, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Uhamiaji chini ya Hamad Masauni, Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais Tamisemi chini ya Angellah Kairuki na Mamlaka ya Mapato (TRA).
Rais Samia aliyekuwa akihitimisha maadhimisho ya sikukuu ya wakulima, Nanenane yaliyofanyika katika viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya, leo Agosti 8, 2023 amesema mfumo huo utaiwezesha Serikali kukusanya fedha na kudhibiti wafanyabiashara wasio waaminifu.
“Tunataka tuwe na mfumo rasmi wa ununuzi, uuzaji na usafirishaji wa mazao yetu, utaratibu huo utatuwezesha kufahamu kiasi cha mazao yanayouzwa nje na fedha inayopatikana ili kudhibiti wafanyabiashara wasio waaminifu,” ameongeza Rais Samia.
Mbali na kudhibiti wafanyabiashara wasio waaminifu Rais Samia amesema Serikali yake itadhibiti uuzaji holela wa mazao ili kunufaisha wakulima wanaotengemea shughuli hiyo kujipatia kipato.
Kauli ya Rais Samia inakuja baada ya kuwepo kwa malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa baadhi ya wafanyabiashara kuzuiwa kusafirisha mazao nje ya nchi na jambo hilo limesababisha kuporomoka kwa bei ya mahindi.
Itakumbukwa Juni 22, 2023 Mbunge wa Mbozi, George Mwenisongole alimuomba Spika wa Bunge Tulia Ackson kujadili kwa dharula zuio la Serikali la kusafirisha mazao nje ya nchi jambo lililosababisha kuporomoka kwa bei ya mahindi na kufikia Sh7,000 kwa kilo 20 ambapo Waziri wa Kilimo Hussein Bashe alifafanua kuwa kilichozuiwa ni usafirishaji holela wa mazao ambapo Serikali inaandaa mfumo maalumu.
Soma zaidi
-
Rais Samia: Watu milioni 51.3 wanakabiliwa na upungufu wa chakula SADC
-
Bajeti ya Wizara ya Kilimo yaongezeka kwa asilimia 29
Awali Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amewahakikishia wakulima kuwa Wizara yake kupitia Wakala wa Uhifadhi wa Chakula imejipanga vyema kunununua mazao ya wakulima kwa bei nzuri itakayowawezesha wakulima kupata faida.
“Nataka niwahakikishie wakulima mama amefungua pochi NFRA ina fedha CPB ina fedha nendeni mkalime tutaendelea kununua mazao kwa bei competitive (shindani) ambavo itakuwa inafanya wafanyabishara waliokuwa wananunua mazao kwa Sh200 sasa wanunue kwa bei ya soko halisi,” amesema Bashe.
Katika hafla hiyo ya kilele cha sikukuu ya wakulima Rais Samia ametembelea mabanda mbalimbali ya wakulima, wafugaji na wavuvi walioshiriki katika maonesho ya sikukuu hiyo kujionea jitihada, ubunifu na maendeleo ya shughuli wanazozifanya.
Pia amezindua uchimbaji wa visima 67,850 ambapo kila kisima kimoja kinatarajiwa kuhudumia wakulima wadogo 16 ambao pia watapewa ekari 2.5 za seti ya umwagiliaji(irrigation set).
Latest
