Rais Samia aongoza kikao cha kwanza cha Tume ya Mipango
- Tume hiyo inaundwa na wajumbe sita akiwemo Waziri wa Fedha Dk Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo.
- Asema kuwa tume hiyo itakidhi kiu na maratajio ya Watanzania katika kuwa na mipango ya pamoja na maendeleo jumuishi.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan ameongoza kikao cha kwanza cha Tume ya Mipango yenye dhamana ya kusimamia uchumi, upangaji na utekelezaji wa mipango ya maendeleo nchini.
Kikao hicho kimehudhuriwa na wajumbe sita ambao ni Waziri wa Fedha Dk Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, Omar Issa, Balozi Ombeni Sefue, Balozi Ami Mpungwe na Balozi Asha-Rose Migiro.
Kabla ya kikao hicho Rais Samia aliwaapisha wajumbe hao ambao kwa mujibu wa Sheria ya Tume ya Mipango ya mwaka 2023 kifungu cha 5 (4) wajumbe hao watakaa madarakani kwa kipindi cha miaka mitano na wanaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine kimoja.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza katika kikao hicho leo Mei 29, 2024 Ikulu mkoani Dodoma amesema kuwa tume hiyo imebeba dhamana kubwa na imani yake ni kwamba itakidhi kiu na maratajio ya Watanzania katika kuwa na mipango ya pamoja na maendeleo jumuishi.
Soma zaidi:Zingatia haya kabla hujafungua kesi ya madai mahakamani
Aidha, ameitaka tume ijitahidi kutathmini ubora wa miradi mbalimbali inayoendelea ili iwanufaishe wananchi kwa jumla na kutumia rasilimali chache kuleta matokeo makubwa.
Katika hatua nyingine, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa matumizi ya takwimu na tafiti kwenye kufanya maamuzi katika tume hiyo inayosaidiwa na Sekretarieti ya Tume ya Mipango ikiongozwa na Katibu Mtendaji.
Tume hiyo pia inawajibika kuandaa mpango mkakati ili kufungamanisha utekelezaji wa majukumu yake na Dira ya Taifa ya Maendeleo na kuishauri Serikali kuhusu mipango ya maendeleo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiwa kwenye picha ya pamoja na Wajumbe wa Tume ya Mipango mara baada ya kuwaapisha na kuzungumza nao katika hafla fupi iliyofanyika Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 29 Mei, 2024.Picha|Ikulu Mawasiliano.
Mbali na majukumu hayo, Sheria ya Tume ya Mipango ya Mwaka 2023 inayataja majukumu mengine ya tume hiyo kuwa ni pamoja na kufanya tathmini na uchambuzi wa mara kwa mara wa viashiria muhimu vya uchumi ambavyo vinajumuisha urari wa malipo,mtiririko wa fedha na bei, deni la Taifa na kuishauri Serikali ipasavyo.
“Kufuatilia utekelezaji wa maeneo muhimu ya vipaumbele vya taifa kwa sekta mbalimbali za uchumi na kuhakikisha kuwa hatua stahiki zinachukuliwa ili kutatua changamoto zozote za uendeshaji zitakazobainika katika sekta hizo,” imebainisha Sheria hiyo.