Rais Samia amteua bosi mpya wa Usalama wa Taifa
- Ni Balozi Ali Idi Siwa.
- Anachukua nafasi ya Massoro aliyeteuliwa kuwa Balozi.
- Huu ni uteuzi wa pili wa kiongozi wa juu wa taasisi hiyo nyeti nchini ukifuatia ule wa Januari 3, 2023.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amemteua Balozi Ali Idi Siwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (Tiss) na kumuapisha leo Ikulu jijini Dar es Salaam.
Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu leo Agosti 28, 2023 na kusainiwa na Mkurugenzi wake Zuhura Yunus imeeleza kuwa Balozi Siwa anachukua nafasi ya Hussein Massoro ambaye ameteuliwa kuwa balozi.
“Balozi Siwa ameapishwa leo tarehe 28 Agosti, 2023 Ikulu jijini Dar es Salaam na anachukua nafasi ya Said Hussein Massoro ambaye ameteuliwa kuwa Balozi,” inabainisha taarifa hiyo.
Massoro ambaye awali alikuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu na Mkurugenzi wa Shughuli za ndani wa Tiss, ameteuliwa kuwa balozi baada ya kuhudumu katika nafasi hiyo kwa siku 238 akichukua nafasi ya Diwani Athumani ambaye aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu Ikulu.
Huu ni uteuzi wa pili wa kiongozi wa juu wa taasisi hiyo nyeti nchini ukifuatia ule wa Januari 3, 2023.
Latest
