Rais Samia afanya uteuzi, mabadiliko wizara mbili
- Uapisho wa viongozi hao utafanyika katika tarehe itakayopangwa.
Arusha. Rais Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi, uhamisho wa viongozi mbalimbali Serikalini pamoja na mabadiliko ya muundo katika Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji na Wizara ya Nishati.
Taarifa ya Bakari Machumu, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu iliyotolewa usiku wa leo Februari 6, 2026 inabainisha kuwa mabadiliko hayo yaliyofanywa katika wizara hizo yatafanya idadi ya makatibu wakuu katika wizara hizo kuwa wawili kwa kila wizara.
“Dk Tausi Mbaga Kida ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dk Fred Matola Msemwa ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Uwekezaji,” imesema taarifa ya Machumu iliyorejea taarifa ya Katibu Mkuu Moses Kusiluka.
Wengine walioteuliwa kujaza nafasi hizo mbili katika Wizara ya Nishati ni Dk James Peter Mataragio ambaye atashughulikia masuala ya mafuta na gesi asilia na Mhandisi Felchesmi Jossen Mramba atashughulikia masuala ya umeme na nishati jadidifu.
Kabla ya uteuzi huo Dk Mataragio alikuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, nafasi aliyoitumikia kwa miaka miwili tangu Februari, 2024.
Rais Samia pia amemteua Balozi Waziri Rajab Salum kuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Viwanda na Biashara akichukua nafasi ya Dk Hashil Twaib Abdallah ambaye atapangiwa majukumu mengine.
Katiika hatua nyingine kiongozi huyo wa nchi amefanya uteuzi wa naibu katibu mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Balozi, mwenyekiti wa bodi, wakuu wamikoa wawili, makatibu tawala wa mikoa wawili na naibu makatibu wakuu nane.
Aidha, uapisho wa viongozi hao utafanyika katika tarehe itakayopangwa.
Latest