Maagizo ya Rais Samia kwa wateule wapya
- Awataka kufanyia kazi ripoti ya CAG.
- Asema mabadiliko ya viongozi Serikalini ni ya kawaida.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amewaapisha viongozi wateule wakiwemo makatibu wakuu na wakuu wa mikoa huku akiwaagiza kufanya kazi kwa ufanisi na kutatua migogoro katika vituo vyao vipya vya kazi.
Rais Samia ametoa maagizo hayo leo Aprili 4, 2024 Ikulu jijini Dar es Salaam ilipofanyika hafla ya kuwaapisha wateule hao aliowateua jana.
Miongoni mwa walioteuliwa ni pamoja na Paul Makonda aliyekuwa Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ambaye amekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Sylvester Kainda aliyeteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mhandisi Mary Prisca Mahundi aliyeteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.
Rais Samia amesema kuwa mabadiliko aliyoyafanya ni ya kawaida na kwamba kazi kubwa waliyonayo ni kuunganisha watu na kutatua migogoro ya wananchi.
“Mabadiliko haya ni mambo ya kawaida, kubwa ni kuimarisha ufanisi katika kutoa huduma kwa wananchi wetu, niwaombe kafanyeni kazi kwa kuwaunganisha watu, nendeni katatueni migogoro msiende kutengeneza migogoro,” amesema Rais Samia.
Soma zaidi: Serikali kufumua sera za uwekezaji, viwanda Tanzania
Rais Samia amemuagiza Makonda kusimamia shughuli za kiutalii zinazoendelea katika Mkoa wa Arusha ili ziweze kuongeza pato la Taifa.
“Tumekupeleka Arusha kwa sababu unajua nini kipo Arusha na unajua matumaini yangu kwako…Kubwa Arusha ni utalii, wageni ni wengi malazi hakuna nenda kasimamie ukishirikiano na wawekezaji,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia ametoa maagizo mengine kwa wateule hao hususani katika Wizara ya Habari, Mawasiliano na Taeknolojia ya Habari kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa namba moja (namba jamii) itakayowezesha Watanzania kutambuliwa katika huduma mbalimbali huku ikiimarisha usalama.
Ripoti ya CAG kufanyiwa kazi
Katika maagizo yake kwa viongozi wapya hii leo Rais Samia amewataka kufanyia kazi ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hessbu za Serikali (CAG) Charles Kichere ya mwaka 2022/2023 iliyowasilishwa kwa Rais Machi 28, 2024 jijini Dar es Salaam.
“Hii ni kwa mawaziri wote mliopo, ripoti ya CAG ikasimamiwe, ikafanyiwe kazi, hoja zile zijibiwe ‘immediately’(haraka)…mkijibu immediately tutajua yapi yamejibika yapi hayajajibika na hatua gani zichukuliwe,” amesema Rais.
Kauli hii ya Rais Samia inakuja wakati ambapo kumekuwa na maoni tofauti katika mitandao ya kijamii huku baadhi ya watu wakisema mapendekezo ya ripoti ya CAG hayatekelezwi na wahusika waliobainika kufanya ubadhirifu wa fedha ya Serikali hawachukuliwi hatua.