Pato la Mtanzania lapaa kwa Sh97,185 mwaka 2021

June 14, 2022 8:56 am · David
Share
Tweet
Copy Link
  • Serikali yasema ukuaji huo umechochewa na jitihada za kuboresha maisha ya watu kiuchumi.
  • Jitihada hizo ikiwemo utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO–19.
  • Shughuli za kiuchumi zilizokuwa na ukuaji mkubwa mwaka 2021 nii pamoja na Sanaa na Burudani.

Dar es Salaam.  Wastani wa pato la mtu kwa mwaka nchini Tanzania umeongezeka kwa Sh97,185 ndani ya mwaka mmoja huku Serikali ikieleza kuwa ukuaji huo umechochewa na jitihada za kuboresha maisha ya watu kiuchumi. 

Dk Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango amewaeleza wabunge jijini Dodoma leo (Juni 14, 2022) kuwa wastani wa pato kwa mtu ulifikia Sh2.798 milioni mwaka 2021 kutoka Sh2.701 milioni mwaka 2020. 

Kiwango hicho, kwa mujibu wa Dk Nchemba kwa hesabu za fedha za kigeni, kimeongezeka hadi Dola za Marekani 1,211.77 mwaka 2021 kutoka Dola za Marekani 1,171.51 mwaka 2020.

Dk Nchemba, aliyekuwa akisoma Taarifa ya hali ya uchumi wa Taifa kwa mwaka 2021 na Mpango wa maendeleo ya Taifa wa mwaka 2022/23, amesema uchumi wa Taifa ulikua kwa asilimia 4.9 mwaka 2021 ikiwa ni juu kidogo ya ukuaji wa asilimia 4.8 uliorekodiwa mwaka 2020. 

Hata hivyo, ukuaji huo wa uchumi wa mwaka 2021 ulikuwa chini kidogo ya lengo la asilimia 5 katika mwaka 2021 kwa mujibu wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT). Baadhi ya wakazi wa Kigoma Ujiji wakishona mashuka kwa ajili ya kuyauza sokoni mwishoni mwa Juni 2021. Ukuaji chanya wa kiuchumi husaidia watu wengi kujikwamua na umaskini. Picha|Maktaba.

Dk Nchemba amesema Pato Ghafi la Taifa (GDP)  lilikua hadi Sh161.5 trilioni mwaka 2021 kutoka Sh151.2 trilioni  mwaka 2020 zikichochewa zaidi na ukuaji wa shughuli za kiuchumi kama sanaa na burudani, umeme, uchimbaji madini na mawe. 

Katika kipindi hicho cha mwaka 2021, waziri huyo amesema Tanzania Bara ilikuwa inakadiriwa kuwa na watu milioni 57.7 ikilinganishwa na watu milioni 55.9 mwaka 2020. 

Kukua kwa uchumi, Dk Nchemba amesema kulichochewa na jitihada za utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO–19 na uwekezaji wa kimkakati hususan katika miundombinu ya nishati, maji, afya, elimu, ujenzi wa barabara, reli na viwanja vya ndege.

“Shughuli za kiuchumi zilizokuwa na ukuaji mkubwa katika kipindi cha mwaka 2021 ni pamoja na Sanaa na Burudani (asilimia 19.4), Umeme (asilimia 10.0), Uchimbaji Madini na Mawe (asilimia 9.6) na Habari na Mawasiliano (asilimia 9.1),” amesema Dk Nchemba.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW