Njia zitakazosaidia biashara kupata faida kubwa, kudumu muda mrefu
- Jifunze kuweka rekodi ya matumizi yako na kuwa na menejimenti nzuri itakusaidia kuongeza nguvu ya kufanya vizuri katika kampuni yako.
- Anza kupanga mikakati ya nani ataendeleza kampuni hata usipokuwepo ili iweze kudumu kwa muda mrefu zaidi.
- kuwa na uwezo wa kukabili matumizi yako ili uweze kujua njia nzuri ya kutunza fedha.
Dar es Salaam. Kila mjasiriamali au mfanyabiashara ndoto yake kubwa ni kuona kampuni yake inakua na kudumu kwa muda mrefu.
Mbali na kukua, kampuni inatakiwa ilete faida mwaka hadi mwaka ambayo itaiwezesha kujiendesha yenyewe bila kutegemea fedha zaidi mfukoni za mwekezaji au mwanzilishi wake.
Safari ya kuifanya kampuni ijiendeshe yenyewe na kuzalisha faida siyo ya kitoto. Ni safari ya machozi na damu.
Baadhi ya wazoefu na waliofanikiwa katika uendeshaji wa biashara wamekuwa wakitoa mbinu ambazo zitasaidia biashara changa kukua na hatimaye kuanza kutengeneza faida.
Katika wasilisho maalum kwa wajasiriamali Februari 21, 2019, Ofisa Mkuu wa Fedha toka benki ya biashara ya UBA, Chomete Hussein alitoa mbinu muhimu kwa wajasiriamali hao jinsi ya kuendesha kampuni au biashara ili iweze kuleta faida
Jifunze kuweka rekodi
Hussein amewashauri wajasiriamali hao kuwa na tabia ya kurekodi vitu mbalimbali wanavyofanya ili waweze kujua mwenendo wa biashara zao na wapi wanakwama na kwa kiasi gani wanaweza kujisahihisha ili waweze kusonga mbele. Kila taarifa ya mapato na matumizi iwekwe kwenye kumbukumbu vizuri.
“Unatakiwa upange vitu vizuri, kuwa na mfumo wa benki na tunza kumbukumbu zako inaweza hata kushawishi watu kuwekeza,” amesema Hussein.

Wajasiriamali wa kampuini changa wakimsikiliza kwa ukaribu na Chomete Hussein akiwapa mbinu za kufanya kampuni zao kukua katika mkutano uliowakutanisha Seedspace jijini Dar es Salaam. Picha| Zahara Tunda.
Kuwa na menejimenti nzuri
Hapa anasema kuwa ni lazima kampuni iwe na menejimenti nzuri na yenye watu wanaojua taaluma zao ili kuleta ufanisi katika kazi.
Anasema kuwa unaweza kuwa na mawazo mazuri ya kibiashara lakini ukawa hauna uwezo wa kuendesha vizuri hivyo ni vyema ukawaajiri watu wanaoweza kuifanya na wewe ukabaki kuwa msimamizi ili mwisho wa siku uweze kukua kibiashara.
Kuwa na uwezo wa kukabili matumizi
Hussein anashauri wajasiriamali wawe na uwezo wa kukabili matumizi katika uendeshaji wa biashara zao. Unatakiwa ujue matumizi yako yapoje na ulitumia wapi kwa misingi gani na unawezaje kuirudisha pesa hiyo.
“Usipoweka kumbukumbu utaishia kusema chuma ulete,” amesema Hussein.
Vilevile kwenye biashara, anasema hata kama ulitoa pesa kwa mambo binafsi inapaswa iandikiwe na kuwe na namna ya kupima mahesabu.
Zinazohusiana: Unayafahamu majukumu aliyonayo mwekezaji kwenye ‘startups’?
Utambulisho, uwekezaji kuzibeba ‘Startups’ Tanzania
Tabia ya baadhi ya wajasiriamali kutumia fedha kwa matumizi bila kurejesha fedha hizo baadaye si rafiki na inaua biashara haraka.
Kwa uzoefu, Hussein anasema mwanzo wa biashara pesa huwa inayotumika zaidi kuliko iliyotoka lakini kama ukiendelea kuwa na matumizi mengi bila faida inapaswa uanze kufikiria unakosea wapi.

Wafanyabiashara wanaochipukia kwenye kampuni changa hawana budi kusaka maarifa zaidi ili waweze kufikia malengo yao.Picha| Zahara Tunda.
Kuwa na mbinu za kukabidhisha kampuni kwa wengine ili iweze kuendelea zaidi
Hapa mtaalam huyo anawashauri wajasiriamali wenye kampuni changa kuwa na mipango endelevu juu ya kampuni zao kwa sababu wengi wanakufa na kampuni kutokana na kutokuwa na mazoea ya kujiandaa vizuri kwa ajili ya kukabidhi kwa wengine.
Mfano, anasema benki ya UBA imeweza kukaa miaka zaidi ya 70 kwa sababu wapo watu wanaoindeleza alipoishia mwanzilishi.
“Kama mjasiriamali uwe na uwezo wa kumpa mtu mwingine mawazo ili yaweze kudumu,” amesema Hussein.
Hata hivyo, anaeleza wazi kuwa yote hayo yatawezekana kama tangu siku ya kwanza utaweza kutambua mshahara wako ni upi na unawezaje kuwa na mzunguko wa pesa utakaoweza kuleta maslahi katika kampuni yako.