Mwelekeo mpya mapambano magonjwa ya milipuko duniani
- Wanasayansi kujichimbia kufuatilia vimelea vya magonjwa hayo.
- Magonjwa kama Uviko-19, Ebola na Marbug kupewa kipaumbele.
Dar es salaam. Wakati mataifa mbalimbali duniani yakiendelea kukabiliana na magonjwa ya milipuko ambayo yamesababisha athari nyingi kiuchumi na kijamii ikiwemo Uviko-19 na Ebola, wanasayansi wanafikiria kuja na suluhu ya kuepusha kabisa magonjwa hayo kwa siku za usoni.
Kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa kwenye tovuti ya Shirika la Afya Duniani (WHO) jana Jumatatu Novemba 21, 2022, shirika hilo lipo mbioni kuzindua mchakato wa kufuatilia vimelea ambavyo vinaweza kusababisha magonjwa ya milipuko.
Ufuatiliaji huo utafanywa na jopo la wanasayansi zaidi ya 300 ambao watafuatilia familia za bakteria na virusi 25 na kisha watapendekeza ni vimelea vipi vipewe kipaumbele zaidi.
Soma zaidi:
Mchakato huo utahusisha vigezo vya kisayansi vinavyohusiana na athari za kijamii na kiuchumi ambapo unatarajiwa utachochea maendeleo ya tafiti katika upatikanaji wa tiba pamoja na chanjo.
“Ni muhimu kuwa na mchakato huu hususan linapotokea janga linalohitaji majibu ya haraka kama Uviko-19, isingekuwa rahisi kupambana nao kwa haraka kama kusingekuwa na hatua kama hizi,” anasema Dk Michael Ryan, Mkurugenzi wa Mpango wa Dharura wa WHO.
Magonjwa kama Ebola, Uviko-19, Marbug, homa ya Lassa, homa ya bonde la ufa pamoja na zika ni miongoni mwa maradhi yaliyopo katika orodha ya magonjwa yatakayopewa kipaumbele katika utafiti huo.
Latest