‘Mfalme’ Zumaridi kufikishwa mahakamani

February 28, 2022 1:57 pm · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Polisi waendelea na upelelezi, ukikamilika atafikishwa mahakamani.
  • Amekuwa akiwaaminisha watu kuwa yeye ni Mungu anayeponya, kufufua watu na kutatua matatizo yao.
  • Ni mkazi wa Mtaa wa Buguku, Diana Bundala (39). 

Mwanza. Jeshi la Polisi mkoani Mwanza limesema linakamilisha upelelezi wa kesi inayomkabilia mkazi wa Mtaa wa Buguku, Diana Bundala (39)  maarufu kwa jina la Mfalme “Zumaridi” ili afikishwe mahakamani.

Mfalme Zumaridi alikamatwa  February 26, 2022 akituhumiwa kwa kosa la usafirishaji haramu wa binadamu 149. 

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ramadhan Ng’anzi amesema watu wanadaiwa kusafirishwa, kati yao, wanawake ni 92 na miongoni mwao ni watoto 24 wanaokadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 4 hadi 17 ambao wamekatizwa masomo yao kinyume na sheria.

“Upelelezi wa kina unaendelea ili kubaini kiini cha watu hao kukusanyika katika nyumba ya mtuhumiwa ambayo siyo nyumba ya ibada wala sehemu rasmi ya kongamano baada ya upelelezi kukamilika mtuhumiwa pamoja na wafuasi wake atafikishwa mahakamani  ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa,” amesema Ng’anzi.

Kamanda Ng’anzi amesema Mfalme Zumaridi amekuwa akiwaaminisha kuwa yeye ni Mungu anayeponya , kufufua na kutatua matatizo yao.

Zumaridi alikamatwa baada ya polisi kupokea amri ya Mahakama ya Mwanzo Mkuyuni  Februari 23 mwaka huu iliyotaka kumkamata mzazi wa kike wa mototo Samir Abbas aliyetakiwa kufikishwa mbele ya mahakama hiyo baada ya kesi ya msingi kusikilizwa .

“Katika utekelezaji wa amri hiyo polisi walifika nyumbani kwa mtuhumiwa Diana Bundala ambapo ilidaiwa yupo mzazi wa kike wa mototo huyo na mototo aliyetakiwa kufikishwa mahakamani na baada ya askari hao kufika, aliongoza wafuasi wake na kuanza kuwashambulia askari hao wakiwazuia kufanya kazi yao,” amesema Kamanda Ng’anzi.

Kukamatwa kwa Zumaridi kumekuja ikiwa ni chache baada ya kuonekana kwa video kwenye mitandao ya jamii ikiwaonyesha polisi waliovamia makazi yake wakikabiliana na wafuasi wa mwanamke huyo.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW