Masoud Othman aapishwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar

March 3, 2021 4:03 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link

  • Uapisho huo unafuatia Othman kuteuliwa jana na Dk Mwinyi katika nafasi hiyo ambapo kiongozi huyo anachukua nafasi ya Hayati Maalim Seif aliyefariki dunia Februari 17 mwaka huu.

Dar es Salaam. Rais wa Zanzibar Hussein Mwinyi amemuapisha Othman Masoud Othman kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar leo Machi 2, 2021 Ikulu Zanzibar ili kuanza majukumu yake rasmi. 

Uapisho huo unafuatia Othman kuteuliwa jana na Dk Mwinyi katika nafasi hiyo ambapo kiongozi huyo anachukua nafasi ya Hayati Maalim Seif aliyefariki dunia Februari 17 mwaka huu.

Hafla hiyo ya uapisho ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na hakukuwa na hotuba kutoka kwa viongozi waliohudhuria. 

                               

Jana Machi 1 baada ya kuteuliwa, Othman ambaye aliwahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar alisema kuteuliwa kwake hakumfanyi kuwa sawa na Hayati Maalim seif bali kunampa nafasi ya kuendeleza mapambano ya kupigania umoja, usawa na amani ya Wazanzibari.

“Kamwe sitojipima mezani (mizani) ya Maalim daima sitotimia, bali nitajipima katika mezani ya matarajio ya watu wa Zanzibar na hatma ya nchi yao. Shauku na haki ya maendeleo. Haki ya maridhiano, utulivu na mshikamano. Haki ya kuwa pale wanapostahiki. 

Haki ya kuwa na fahari na nchi yao. Hayo naamini yatapatikana kwa kumsaidia Rais wetu kujenga misingi imara ya taasisi za umma,” inasomeka sehemu ya salamu za Othman katika taarifa ya chama chake cha Chama cha ACT-Wazalendo.

Othman ambaye ni mwanachama wa ACT-Wazalendo ana uzoefu katika kuongoza taasisi mbalimbali za umma visiwani humo zilizomfanya kuaminiwa na Wazanzibar kushika nafasi hiyo ya juu ya uongozi. 

Aliwahi kuwa Mwenyekiti wa mwanzo wa Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) Mwaka 1997, Katibu Mkuu muanzilishi wa Wizara ya Katiba na Utawala Bora.

Mwaka 2000 aliteuliwa kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu katika utawala wa Rais Amani Abeid Karume.


 Soma zaidi: 


Pia mwaka 2002, Rais Karume alimteua Othman kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka wa Mwanzo wa Zanzibar na nyota yake ilizidi kung’aa pale alipoteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar mwaka 2011 na aliyewahi kuwa Rais wa Zanzibar, Ali Mohammed Shein.

Hata hivyo, mwaka 2014 alipoteza nafasi hiyo baada ya kujiuzulu katika nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Uandishi wa Katiba Mpya mwaka 2014 iliyokuwa chini Bunge la Katiba lililokuwa linaongozwa na Hayati Samuel Sitta.

Othman alifikia hatua hiyo baada ya kupendekezwa mambo 17 yenye maslahi kwa Zanzibar yaingizwe ndani ya Katiba iliyopendekezwa na Bunge, lakini yalikatiliwa.

Kutokana na sintofahamu hiyo, iliwalazimu viongozi wa juu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho Othman alikuwa mwanachama kuazimia kufukuzwa kazi kwa mwanasheria huyo kwa kile walichodai amekisaliti chama.

Mwanasheria huyo amerudi tena katika Serikali ya SMZ akiwa siyo mwanachama wa CCM bali wa ACT-Wazalendo.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW