Mambo atakayoshuhudia Samia tamasha la utamaduni Mwanza
- Anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika tamasha la utamaduni.
- Atapata fursa ya kushuhudia matukio mbalimbali ikiwemo ngoma za asili.
- Litafanyika kwa siku mbili kati ya Septemba 7 na 8 mwaka huu katika viwanja vya Red Cross, Kisesa wilayani Magu.
Mwanza. Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika tamasha la utamaduni litakalofanyika mkoani Mwanza na atapata fursa ya kushuhudia matukio mbalimbali ikiwemo ngoma za asili za makabila ya Kanda ya Ziwa.
Tamasha hilo litafanyika kwa siku mbili kati ya Septemba 7 na 8 mwaka huu katika viwanja vya Red Cross, Kisesa wilayani Magu.
Miongozi mwa mambo yatakayofanyika kwenye tamasha hilo ni pamoja na michezo ya jadi kama kurusha mkuki , kucheza bao, kucheza na mti, uandaaji wa chakula kwa njia ya asili na kuandaa moto bila kutumia kiberti (kupekecha).
Pia ngoma za asili za makabila mbalimbali pamoja na namna ya kusimika viongozi wa kimila itakuwa ni miongoni mwa burudani ambazo Rais Samia anatarajia
Katibu wa Umoja wa Machifu wa Kisukuma, Aaron Mikomangwa amesema tamasha hilo linatarajiwa kukusanya machifu zaidi ya 120 kutoka sehemu mbalimbali nchini.
“Katika tamasha hili tutashuhudia mambo kadhaa ya kiutamadauni ikiwemo suala la mavazi, michezo ya jadi, utamaduni wa namna ya kuwasimika viongozi wa makabila na ngoma pamoja na kuona namna akina mama walivyokuwa wakitwanga mpunga kwa kutumia michi mitatu kwenye kinu moja,” amesema Mikomangwa.
Katika tamasha hilo watu watapata fursa ya kuona na kuzungumzia tamaduni zilizo kwenye maeneo yao na uhusiano wake na kijamii ikiwa ni sehemu ya alama mhimu kwa Mtanzania.
Latest
