Serikali kutumia matamasha ya utamaduni kukuza utalii Tanzania
Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Septemba 8, 2021 amesimikwa kuwa chifu wa machifu wakuu Tanzania na kupewa jina la Hangaya. Jina la Hangaya linamaanisha nyota inayong’ara. Picha| Mariam John.
- Yaagiza matamasha hayo yafanyike mikoani kila mwaka.
- Rais Samia asema yatasaidia kutangaza utalii wa kiutamaduni.
Mwanza. Huenda idadi ya watalii wanaotembelea Tanzania ikaongezeka kila mwaka, baada ya Rais Samia Suluhusu Hassan kuagiza matamasha ya utaduni kufanya kila mkoa ili kutangaza mila na desturi za Watanzania.
Tanzania imejiwekea malengo ya kufikisha watalii milioni 5 kwa mwaka ifikapo mwaka 2025. Ili kufikia lengo hilo inaboresha miundmbinu ya utalii, kutangaza vivutio vilivyopo katika majukwaa mbalimbali yakiwemo matamasha.
Rais Samia ametoa agizo hilo leo Septemba 8, 2021 mkoani Mwanza wakati akifunga tamasha la utamaduni lililoandaliwa na umoja wa machifu nchini ambalo limenga kutangaza vivutio na fursa za kitalii kupitia mila na tamaduni za Kitanzania.
“Nitumie fursa hii kwenu nyinyi machifu kuhakikisha mnalinda maadili ya Mtanzania nimetoa wito kwa matamasha haya kufanyika kuzunguka kila mkoa na nitaenda mbali sana kama Hangaya kushindanisha matamasha haya.
“Nitakuwa na kikombe maalum kwa mkoa utakaofanya vizuri ila kwa kuwa tamasha hili ni la kwanza sitakuwa na kikombe ila nitakuwa za zawadi maalum ambapo kiongozi wa machifu watakuja kuichukua,” amesema Samia.
Kiongozi huyo wa nchi amesema kumekuwepo na wigo mdogo wa wageni wanaofika nchi kutalii kukaa muda mrefu na hiyo ni kutokana kutokuwepo kwa utalii wa utamaduni.
Amesema utalii ni biashara kwa nchi zilizoendelea kwa kuwa zimeweka nguvu kuhakikisha zinaenzi tamaduni zao pamoja na kujitangaza.
“Hayati Mwalimu Julius Nyerere alisema utamaduni ni kiini au roho ya mtu yeyote hivyo tunapaswa kulinda na kuenzi tamaduni zetu kwa ajili ya vizazi vijavyo,” amesema Rais.
Amesema kutokana na changamoto hiyo Serikali imejipanga kutangaza utalii kupitia mila za makabila yote 120 nchini.
Tamasha hilo halitofautiana na lile la ‘Urithi Wetu’ ambalo lilianza kufanyika mwaka 2018 likiwa na linalenga kuenzi na kutangaza utamaduni wa kitanzania duniani.
Shughuli zitakazofanyika katika tamasha hilo ni ngoma na muziki wa asili, mapishi ya vyakula vya kitanzania, maonyesho ya zana za utamaduni na vivutio vingine vya utalii.
Awali Chifu wa Mkoa wa Mwanza, Aron Mikongwa alimuomba Rais Samia kuboresha maeneo ya machifu ikiwemo nyumba za machifu zilizopo Malya wilayani Kwimba, vituo vya makumbusho ya Wasukuma ambavyo vinahitaji maboresho makubwa.
“Machifu tumepoteza umiliki wa nyezo na umiliki wa majengo tuliyokuwa tunayotumia, machifu hatuna urahisi wa kupata nyara za Serikali tunazozitumia kila siku kama usinga tukimaanisha kuongoza watu,” amesema Mikongwa.
Rais Samia ameahidi kushughulikia masuala hayo ili kuhakikisha utamduni wa Mtanzania unaenziwa vizuri.