Mama amzika mwanae akiwa hai ili ajipatie utajiri
- Adanganywa na mganga wa jadi mkoani Mwanza
Mwanza. Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza linawashikilia watu watatu akiwepo mganga wa jadi wakazi wa Kijiji cha Mahaha wilayani Magu kwa tuhuma za mauaji baada ya kudaiwa kumzika mtoto mchanga mwenye umri wa miezi miwili akiwa hai.
Kamanda wa Polisi mkoani humo, Wilbroad Mutafungwa amewataja waliokamatwa kuwa ni pamoja na mama mzazi wa mtoto huyo Zawadi Msagaja na dada yake Elizabeth Kaswa pamoja na Mussa Mazuri ambaye ni mganga wa jadi anayedaiwa kuwarubuni ndugu hao kutekeleza kitendo hicho ili kujipatia utajiri.
Kamanda Mtafungwa amesema tukio hilo lilitokea Novembar 13 mwaka huu ambapo mwanamke huyo alikubali kumtoa mtoto wake kafara ili yeye asife ndipo shemeji yake ambaye ni mganga wa kienyeji kwa kushirikiana na mkewe ambaye ni Elizabeth Kaswa walianza kumpa dawa za kienyeji mtoto na baadae mtoto alianza kukosa nguvu.
“Ilipofika muda wa saa 20:00 usiku wote watatu wakiwa na mtoto huyo walikwenda shambani na kuchimba shimo kisha kumzika akiwa hai na baadaye walirudi nyumbani,” amesema Mtafungwa.
Amesema Jeshi la Polisi lilipata taarifa kutoka kwa wasamaria wema kuhusiana na tukio hilo ndipo ufuatiliaji wa haraka ulifanyika na kufanikiwa kumkamata mama wa mtoto huyo pamoja na dada yake na Novemba 21 mganga huyo alikamatwa katika Kijiji cha Nyagunge wilayani Magu.
Baada ya watuhumiwa hao kukamatwa waliongozana na askari hadi eneo walipozika kichanga hicho na baada ya kufukua kaburi walifanikiwa kuukuta mwili wa mtoto ukiwa umefungwa kanga.
Mwili wa mtoto ulipelekwa hospitali ya Rufaa ya Bugando kusubiri uchunguzi wa daktari.
Kamanda Mtafungwa ametoa onyo kwa wananchi kuacha kutafuta utajiri kwa njia za ushirikina badala yake wafanye kazi kwa bidii ili kujipatia mali.
Latest