Mafunzo kwa watoa huduma yatakavyopaisha utalii Tanzania
- Yanatolewa na Serikali kwa wadau na watoa huduma za utalii.
- Mafunzo hayo yanahusu kuhudumia watalii kwa viwango vya kimataifa.
- Tanzania inakusudia kuongeza watalii milioni 5 ifikapo mwaka 2025.
Mwanza. Huenda idadi ya watalii wanaoendepelea Tanzania kila mwaka ikaongezeka kwa kasi baada ya Serikali kutekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo kutoa mafunzo kwa wadau na watoa huduma za utalii.
Baada ya kuyumba kwa sekta ya utalii nchini wakati wa Uviko-19, chuo cha Taifa cha Utalii Tanzania (NTC) kimeanzisha mafunzo kwa wadau na watoa huduma za utalii ili kuboresha huduma zinazotolewa na sekta hiyo na kuimarisha ushindani katika masoko ya kimataifa.
Mkurugenzi Mtendaji wa chuo hicho, Dk Shogo Mlozi akizungumza katika mafunzo yanayoendelea jijini Mwanza ambayo yamejumuisha wadau na watoa huduma za utalii zaidi ya 150, amesema mchango wa sekta ya utalii ulishuka baada ya janga la Uviko-19 kuingia nchini mwaka 2019.
Amesema mafunzo hayo yamelenga kupandisha kiwango cha watalii kilichopo kwa sasa na kufikia watalii milioni 5 ifikapo mwaka 2025.
“Baada ya kuingia kwa ugonjwa wa Uviko-19 idadi ya watalii ilishuka kutoka watalii milioni 1.5 mwaka 2019 na kufikia watalii 620,867 mwaka 2020 sawa na asilimia 59.3.
“Mpango ulipo ni kupandisha kiwango hiki ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha wadau na watoa huduma katika sekta hiyo waweze kusaidia kwenye mpango huo,” amesema Dk Mlozi.
Zinazohusiana:
- Tanzania yaangazia masoko 18 duniani kukuza utalii
- Tanzania yang’ara tena tuzo za eneo bora la utalii duniani
Amesema pamoja na ugonjwa wa Uviko-19 kuwepo lazima shughuli za uzalishaji katika sekta ya utalii kwa mtu mmoja mmoja ziendelee ili kuimarisha uchumi wa Taifa.
Amesema wadau wanaweza kuboresha vivutio vya utalii na huduma zake ili zivutie watalii kutoka maeneo mbalimbali duniani.
“Huduma kwa wateja ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha anasaidia katika kuiboresha sekta hii ili kufikia azma hii ya kuongeza idadi ya watalii nchini,” amesema Dk Mlozi.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Magu, Salum Kali amesema janga la Uviko-19 lilichangia kuyumba kwa sekta ya utalii duniani ambapo kwa upande wa Tanzania lilisababisha idadi ya watalii kupungua.
“Kupungua kwa wateja hao pia kulisababisha fedha za kigeni kupungua kwa asilimia 20 na fedha za kitaifa kupungua kwa asilimia 17,” amesema Kali.
Amesema wameshuhudia kuyumba kwa biashara za utalii hasa kufungwa kwa baadhi ya makampuni ya utalii na hoteli lakini kwa sasa angalau sekta hiyo imeanza kuimarika.
Mkuu huyo wa Wilaya amesema kujenga uwezo wa namna bora ya kukabiliana na Uviko-19 kwa watoa huduma kutasaidia kuzingatia matakwa ya afya na usalama lakini pia kuleta ushindani wa kimataifa katika kuleta watalii wengi nchini.
“Hali hiyo itasaidia watalii kuiona Tanzania kuwa sehemu salama,” amesema Kali.
Kali amewataka wadau kutoridhika na fukwe ya Ziwa Victoria pekee pamoja na mbuga ya wanyama ya Saanane bali wabuni vyanzo vingine vya mapato atika sekta hiyo.
“Tunaloliziwa hapa, mnaweza kulitumia kutengeneza fukwe ndani ili watalii wanapokuja badala ya kuunganisha mbuga ya wanyama ya Serengeti wapumzike kwenye fukwe za zilizopo Ziwa Victoria, lazima tuwe wabunifu,” amesema Kali.