Kwanini baadhi ya watu wanasita kupata chanjo ya Uviko-19?
- Baadhi yao wameathirika na taarifa za uongo za mtandaoni kuhusu chanjo ya Corona.
- Wengine wanahoji usalama wa chanjo hizo licha ya wataalam wa afya kusema hazina shida kiafya.
- Taarifa sahihi juu ya kiwango cha chanjo kudhibiti Corona hazijawafikia.
Dar es Salaam. Mitandao ya kijamii kwa sasa imekuwa ni kama mahakama ya baadhi ya Watanzania. Inatumika kwa kuhukumu mambo mbalimbali ikiwemo utolewaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Corona.
Wapo wanaotumia jukwaa hilo kwa ajili ya kuelimisha na kuwahamasisha wakapate chanjo lakini pia wapo ambao kwa kutumia picha za dhihaka na maneno ya kupotosha, wanachochea wengine wasiione maana kamili ya chanjo hiyo.
Wapo wanaoweka picha zikionyesha sehemu za filamu za kutisha ambazo zina mazombi, picha hizo zinawadhihaki watu waliopata chanjo ya kuwa hawatokuwa sawa miaka kadhaa ijayo, taarifa ambayo kwa mujibu wa Kituo cha Kudhibiti Magonjwa cha nchini cha nchini Marekani (CDC), siyo kweli.
CDC inaeleza kuwa chanjo ya Uviko-19 imefanyiwa majaribio na imepitia hatua zote za kutengeneza chanjo na hivyo kuthibitishwa kuwa chanjo inayofaa kutumika na wanadamu.
Mbali na CDC, kwa hali ya kawaida nchi ambazo zimeruhusu kutolewa kwa chanjo zilizopitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kasi ya vifo na maambukizi imeanza kupungua ikilinganishwa na kipindi hakuna chanjo.
Hadi Juni 3, 2021 chanjo sita zimefanyiwa mapitio na kuthibitiswa na WHO kwa ajili kutumiwa na watu ikiwemo ya Johnson & Johnson inayotolewa nchini Tanzania.
Chanjo ningine ni pamoja na AstraZeneca/Oxford, Moderna, Pfizer/BionTech, Sinopharm na Sinovac.
Mathalan, kwa takwimu za WHO, nchi ya Marekani kati ya wiki ya Disemba 28, 2020 hadi Januari 4, 2021 ilirekodi kesi za wagonjwa 508,181 wapya wa Uviko.
Lakini kwa takwimu za nchi hiyo hiyo, za wiki ya Julai 26 2021 hadi Agosti 2, 2021, kesi za wagonjwa wa Uviko-19 zimepungua hadi kufikia watu 163,351 kwa wiki. Anguko la zaidi ya nusu ya kesi zilizokuwa zikiripotiwa mwanzo wa mwaka 2021.
Sababu zilizochangia kupungua kwa maambukizi ni kasi ya utoaji chanjo kwa raia wa nchi hiyo.
Sababu zilizochangia kupungua kwa maambukizi ya Corona kwenye baadhi ya nchi ni kasi ya utoaji chanjo kwa raia wa nchi hiyo. Picha| The Citizen.
Njia panda ya Watanzania
Mara baada ya Tanzania kutangaza kutolewa kwa chanjo nchini tangu mwezi Julai, 2021, kwa baadhi ya Watanzania ilikuwa shangwe huku wengine wakibaki na maswali mengi kichwani juu ya uthabiti na uwezo wa chanjo hiyo.
Maswali hayo na mengine yanatokana na kuwepo habari nyingi za uzushi ambazo zinalenga kuwatisha watu na kuzua taharuki kwenye jamii kuhusu maendeleo ya chanjo duniani.
“Sababu ya (baadhi ya ) Watanzania kuogopa chanjo nikiwemo na mimi ni ile hofu ya kufa au kudhurika baada ya kupata hiyo chanjo,” anasema Nyasu Mtweva ambaye ni Mjasiriamali wa Tabata mkoani Dar es Salaam.
Hata hivyo, nadharia alizonazo Mtweva na watu wengine hazina uhalisia kwa sababu WHO na mamlaka za afya nchini zimefanya uhakiki wa chanjo na kubaini kuwa ni salama na zinatoa uhakika wa mtu kujikinga na Uviko-19.
Kwanini baadhi ya watu bado wanasita kupata chanjo dhidi ya Uviko? Majibu ya baadhi ya Watanzania waliofikiwa na Nukta Habari (www.nukta.co.tz).
Tazama video hii kujua baadhi ya vigugumizi wanavyopata Watanzania.
Latest
