Kupanda bei ya mahindi kulivyowabeba wakulima, wafanyabiashara

July 8, 2022 8:46 am · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Bei ya jumla ya gunia la kilo 100 la mahindi kwa mwaka ulioishia Mei 2022 ilikuwa Sh69,771 ikipanda kutoka Sh43,545 mwaka jana.
  • Sababu ni kuongezeka kwa mahitaji na kupungua kwa mavuno.
  • Bei za mazao mengine ya chakula nazo zapanda.

Dar es Salaam. Wakulima na wafanyabiashara huenda ni miongoni mwa watu walionufaika zaidi na zao la mahindi baada ya bei ya jumla ya zao hilo kupanda kwa Sh26,225 ndani ya kipindi cha mwaka mmoja uliopita. 

Ripoti ya Mapitio ya Uchumi ya Juni 2022 (Monthly Economic Review) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT)  inaeleza kuwa bei ya jumla ya gunia la kilo 100 la mahindi kwa mwaka ulioishia Mei 2022 ilikuwa Sh69,771 ikipanda kutoka Sh43,545 iliyorekodiwa kipindi kama hicho mwaka jana.

Hiyo ni sawa na kusema wakulima na wafanyabiashara wameweka kibindoni Sh26,225 zaidi kwa kila gunia moja ikilinganishwa na bei ya mwaka jana. 

Kupanda kwa bei kunawaumiza walaji kwa sababu wanalazimika kutoboa mifuko yao zaidi ili kupata zao hilo la chakula.

BOT katika ripoti hiyo imeeleza kuwa kupanda kwa bei ya mahindi kumechangiwa na kuongezeka kwa mahitaji ya zao hilo hasa nje ya nchi na kutokuwepo kwa mvua za kutosha katika msimu huu, jambo lililosababisha wakulima wapate mazao kidogo.“Bei za jumla za mazao makuu ya chakula zilikuwa juu Mei ikilinganishwa na mwaka 2021.


Zinahusiana: 


Kuongezeka kwa bei kumechangiwa na mahitaji makubwa ya nchi jirani na kushuka kwa mavuno kutokana na mvua chache,” imeeleza BoT katika ripoti hiyo ambayo inapatikana katika tovuti yake. 

Hata hivyo, bei ya mahindi imekuwa ya kupanda na kushuka tangu mwaka huu uanze ambapo Januari ilikuwa Sh65,864 ikapanda hadi Sh62,326 mwezi uliofuata kabla haijashuka hadi Sh60,996 mwezi Mach.

Aprili bei ikapanda kidogo hadi Sh62,542 kabla haijapanda zaidi hadi Sh69,771 mwezi uliopita wa Mei. 

Mahindi ni miongoni mwa mazao makuu ya chakula yanayojumuisha mchele, maharage, viazi mviringo, mahindi, mtama, uwele, ulezi na ngano ambayo hutumiwa zaidi na Watanzania.

Pia katika kipindi hicho cha mwaka mmoja uliopita bei za mazao mengine ya chakula zimepanda ikiwemo viazi mviringo na mchele.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW