Kampeni za kuwazuia watoto wadogo kutumia simu janja zitafanikiwa?
- Wazazi waanzisha kampeni ya kuishawishi jamii kuwazuia watoto kutumia simu katika umri mdogo ili kuwalinda dhidi ya athari za mtandaoni.
- Tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa mtoto akianza kutumia simu katika umri mdogo, matokeo yake darasani yanashuka.
- Uamuzi wa mzazi kumpa au kumnyima mtoto ruhusa ya kutumia simu unabaki katika uwezo wake kwasababu ana jukumu la kumlea mtoto wake katika malezi ya bora.
Dar es Salaam. Moja ya suala ambalo limeleta changamoto katika malezi ya watoto ni ukuaji wa teknolojia ya mawasiliano hasa matumizi ya simu za kisasa. Mjadala uliopo katika jamii ni umri gani ambao mtoto anaweza kuruhusiwa kutumia simu?
Baadhi ya wazazi wanaona ni sawa mtoto kupewa simu kwasababu anajifunza mambo mazuri kupitia mtandao, lakini kwa wengine wanafikiri simu haina ulinzi na usalama kwa mtoto jambo linaloweza kumuingiza katika mgogoro wa kimaadili asipoongozwa vizuri katika njia sahihi ya maisha yake.
Kutokana na umuhimu wa malezi, wazazi zaidi ya 1,000 kutoka katika majimbo 42 ya Marekani wameanzisha kampeni ijulikanayo “Wait Until 8th Movement” inayokusudia kuwashawishi wazazi nchini humo kutokuwaruhusu watoto wadogo kutumia simu mpaka wafike darasa la nane.
Kampeni hiyo inasambaa kwa kasi katika mitandao ya kijamii ikiwemo Twitter, ilianzishwa na Brooke Shannon, raia wa Marekani na mama wa watoto watatu miezi michache iliyopita ili kuungana na wazazi wengine duniani kuhakikisha watoto hawaathiriwi na mabadiliko ya teknolojia ya mawasiliano na matumizi ya simu.
“Wakati mtoto wangu mkubwa Grace akiwa darasa la awali (kindergarten), watoto kama 5 (katika darasa lao) walikuwa na simu,” ameeleza Shannon wakati akihojiwa na jarida la Chicago Tribune, “Tangu wakati huo imeshuka zaidi hadi kwa watoto wadogo, sasa naona watoto wengi wa madarasa ya awali wana simu za kisasa! Sasa imeenea kote.”
Mzazi mwingine, Shelly Gerson ambaye ameungana na Shannon katika kampeni hiyo amesema kuna madhara mengi ya kiafya na saikolojia yanayoweza kutokea kwa mtoto akianza kutumia simu katika umri mdogo.
“Nina hofu sana kuhusu madhara ya simu kwa maendeleo ya mtoto”, amesema Shelly na kuongeza kuwa, “Sitaki kumuweka mtoto wangu kwenye hatari zaidi za utotoni”.
Shannon anaeleza kuwa kuna kila sababu ya kuwalinda watoto na kuwawekea mipaka katika baadhi ya vitu ikiwemo kutumia simu ambazo zimeunganishwa na intaneti mpaka pale watapokuwa na ufahamu mzuri wa kupambanua mema na mabaya yanayotokea katika ulimwengu wa dijitali.
Zinazohusiana:
- ‘Apps’ za elimu zinavyoweza kuwaelimisha watoto wadogo kabla ya kwenda shule.
- Youtube yaleta mbinu mpya kudhibiti maudhui ya watoto mtandaoni.
Kwanini umzuie mtoto mdogo kutumia simu?
Asili ya mtoto ni utoto yaani kufanya mambo yanayoendana na umri wake ikiwemo kucheza na wenzake, kusoma vitabu, kutumia muda mwingi na familia ili kuhakikisha anajengwa katika mfumo mzuri wa malezi. Lakini simu zilizounganishwa na intaneti zina mchanganyiko wa mambo mbalimbali ambayo mtoto hatakiwi kuyaona au kuyasikia mpaka ifike umri fulani.
Matumizi ya simu janja kwa watoto wadogo yanaweza kuwaweka katika hatari ya kupata tatizo la maadili. Picha| Staanoi
Inavuruga uwezo wake wa kujifunza. Elimu ya awali na msingi ndio msingi wa mafanikio ya kitaalama; mtoto anajifunza jinsi ya kuzalisha, kutunza muda, miradi na kazi za nyumbani. Kumpa simu kunatoa mwanya wa kuzorotesha taaluma na maendeleo yake (academic mediocrity).
Tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa mtoto akianza kutumia simu katika umri mdogo, matokeo yake darasani yanashuka; Utafiti mwingine ulibaini kuwa watoto ambao hawaruhusiwi kuwa na simu shuleni wanafanya vizuri kwenye majaribio ya darasani.
Matumizi ya simu za kisasa na vifaa vingine vyenye mwanga mkali zinaathiri ubora wa usingizi kwa watoto wadogo. Watoto hawapumziki kwasababu wanashawishika kusoma na kujibu ujumbe wa maneno kutoka kwa marafiki zao jambo linalovuruga mpangilio wa kulala wakati wa usiku.
Baadhi ya watoto huamka usiku kuangalia ujumbe au mitandao ya kijamii. Ukosefu wa usingizi kwa watoto unatajwa kuathiri afya ikiwemo ulaji mbaya, unene uliopitiliza, kudhoofisha kinga za mwili, udumavu na magonjwa ya akili.
Ni jambo la kawaida kwa mzazi kuonana mara kwa mara na watoto wake ili kufahamu maendeleo yake na kumuongoza katika njia na mtazamo sahihi wa maisha. Lakini mtoto akitumia simu kwa muda mrefu, mahusiano au ukaribu kwa mzazi wake jambo linalomuweka katika hatari ya kupokea mambo yasiyofaa katika maisha yake.
Inaongeza hatari ya kupata msongo wa mawazo na mkazo. Kwa asili watoto hawana uwezo mkubwa wa kukabiliana na udanganyifu na uhalifu wa kimtandao, ni rahisi kukutana na mambo ambayo yanaweza kumsononesha na kuathiri hisia zake.
Simu janja ni kishawishi cha watoto kuangalia picha za ngono mahali popote walipo. Inaelezwa kuwa watoto hawaishii tu kuangalia picha za ngono bali hutengeneza za kwao na kuzisambaza, jambo linalohatarisha mustakabali wa maisha yao.
Hata hivyo, uamuzi wa mzazi kumpa au kumnyima mtoto ruhusa ya kutumia simu unabaki katika uwezo wake kwasababu ana jukumu la kumlea mtoto wake katika malezi ya bora.