Jinsi unavyoweza kuwadhibiti mende nyumbani

April 29, 2022 11:22 am · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni pamoja na kudhibiti uoshaji wako wa vyombo.
  • Inashauriwa kupulizia dawa ya kuua wadudu walau mara moja kwa mwaka.
  • Vipo vitu ambavyo mende huogopa ikiwemo maganda ya mayai na sukari ya unga.

Dar es Salaam. Changamoto ya wadudu wa nyumbani husababishwa na mengi lakini kubwa zaidi ni hali ya usafi na udhibiti taka katika maeneo yanayozunguka nyumba.

Kuanzia usafi wa makabati, uhifadhi wa vyombo na mpangilio wa vitu nyumbani, ni sababu ya uwepo au kutokuwepo kwa wadudu ambao ni waharibifu ikiwemo mende.

Hali hiyo huwafanya  baadhi kuachana na wazo la kupika hasa kama wanaishi wenyewe wakiogopa uwezekano wa kukaribisha wadudu hao.

Kwa ambao maamuzi yao ya kuanza kupika yamewapatia historia mbaya na mende, makala haya yatawasaidia kupambana na tatizo hilo na kwa ambao wanaanza safari ya kupika pia, wahamasike na njia za kuwaepuka.

Unaweza kudhani ni wadudu tu lakini huenda haufahamu kuwa mende anaweza kusababisha  changamoto za kiafya kwa wakazi na wageni wa nyumbani endapo hawatodhibitiwa.

Tovuti ya masuala ya udhibiti wadudu nyumbani ya Prohealth Pest Control imeandika kuwa, kushindwa kudhibiti mende kunaweza kusababisha ugonjwa wa pumu na kuchochea mzio.

“Mende huacha vichochezi vya mzio hewani kupitia mate, kinyesi na kujivua sehemu za mwili wake (shedding). Haya yanaweza kuathiri mfumo wa upumuaji wa mtu hasa kama ana mzio na pumu,” imeandika Prohealth Pest Control.

Changamoto zigine zilizotajwa ni pamoja na kubeba magonjwa, kuchafua chakula na kuzaliana.

Unawezaje kuwaepuka wadudu hao?

Inashauriwa pia kuziba sehemu ambazo mende wanaweza kuingia ikiwemo nyufa na matobo madirishani. Picha| Big Dave Pate Control.

Epuka kuacha vyombo vichafu vikizagaa

Kama wadudu wengine, mende nao hufika majumbani wakiwa kwenye msako wa msosi. Endapo wakija kwako na wakakuta umeacha vyombo vichafu bila kuviosha, hisia yao ni kama mtu mwenye njaa kufika kwenye ardhi yenye chakula.

Wataweka makazi, watazaliana na kuanza kuwa tatizo nyumbani kwako.

Ili kuepukana na hiyo, inashauriwa kuosha vyombo vyako baada ya kuvitumia hasa muda wa usiku. Usiviache vikizagaa kwenye sinki.

Tumia bidhaa za kufukuza wadudu hasa makabatini

Wakati mwingine hawafuati msosi, wanafuata makazi na mara nyingi, hayo huwa ni chemba za vyooni au makabati.

Ili kuepukana na hali hiyo vipo baadhi ya vitu unavyoweza kuweka kabatini na mende wakakerwa na harufu zake ama uwepo wake.

Vitu hivyo ni pamoja na sukari ya unga, magamba ya mayai na majani yanayojulikana kwa Kiingereza kama  “bay leaves”. Vitu hivi vina harufu ambayo siyo rafiki kwa mende  hivyo hawatokaa makabatini kwako.


Soma zaidi


Weka mbali ndoo ya taka, ifunike kila mara

Mbali na kuvutia nzi nyumbani, ndoo za taka ambazo hazina mifuniko ni kivutio cha paka wa mitaani, nzi na hata wanyama wengine kama vicheche. 

Ndoo ya taka ndani na hata nje ni kivutio pia cha mende hivyo hakikisha kama umeweka ndoo ya taka unahifadhi taka zako kwenye mifuko na mara zote ndoo hiyo inakuwa imefungwa.

Wataalamu wa usafi majumbani, wanashauri kupulizia dawa ya kuua wadudu wa nyumbani walau mara moja kila mwaka.

Tovuti ya heritagepestcontrol imesema kupulizia dawa ni muhimu kwani uonapo mende mmoja nyumbani kwako ni ishara ya kuwa hayupo peke yake. Wapo wenzie wengi waiojificha.

Kupulizia dawa ya wadudu itakusaidia kuwaua kabla hata hawajaanza kukusababishia adha kubwa.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW