Jeshi la Polisi lamsaka mwanamke aliyemywesha mtoto pombe
- Lamtaka ajisalimishe katika kituo chochote cha polisi nchini.
Arusha. Jeshi la Polisi limesema linamtafuta mwanamke mmoja ambaye jina lake halijajulikana anayetuhumiwa kumnywesha pombe mtoto mdogo kinyume na sheria za nchi.
Mwanamke huyo anatuhumiwa kwa kosa hilo bada ya kusambaa kwa picha mjongeo katika mitandao ya kijamii mwishoni mwa wiki hii zikimuonesha akimhamasisha na kumnywesha pombe mtoto mdogo jambo lilotafsiriwa kuwa ni uvunjifu wa sheria na ukatili kwa mtoto.
Sheria hizo ni pamoja na Sheria ya Mtoto Sura ya 13 na Urekebu wa mwaka 2023 kifungu cha 9 (3) na 13 pia ukisoma Sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 na Urekebu wa mwaka 2023 kifungu cha 169 A.
Taarifa ya Msemaji wa Jeshi la Polisi, DCP David Misime iliyotolewa leo Septemba 6, 2025 imeeleza kuwa ufuatiliaji wa tukio hilo pamoja na jitihada za kumpata zimeshaanza.
“Ufuatiliaji wa kina umeshaanza kama tukio hili limetokea ndani ya nchi yetu ili kuweza kumpata huyu aliyekuwa anafanya kitendo hicho kama inavyoonekana kwenye picha mjongeo hiyo…
…Tunamtaka mwanamke huyu akiona taarifa hii ajisalimishe mwenyewe katika Kituo chochote cha Polisi,” imesema taarifa ya Misime.
Aidha, jeshi hilo limetoa wito kwa mtu yeyote anayemfahamu mwanamke huyo kutoa taarifa kwa njia yeyote ile ambayo anaona inafaa na ni rahisi kwake au kupitia namba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi 0699 998899.