Huyu ndiye ‘Valentine’ wako
- Kuacha uovu na mambo yasiyofaa kwenye jamii.
- Tumia muda wako kudumisha upenda na watu wa karibu.
Mwanza. Waumini wa dini ya Kristo na Watanzania wameshauriwa kuacha kuitumia siku ya wapendanao maarufu kama ‘Valentine Day’ kutenda maovu bali kuimarisha mahusiano yao na Mungu ikiwemo kuwasaidia watu wenye uhitaji.
Utamaduni huu ulianzia nchini Roma na kuenea duniani kote. Ulianzishwa ili kumuenzi Padri Valentino ambaye alikiuka katazo la mtawala wa Roma wakati huo Mfalme Claudius II, aliyezuia vijana kufunga ndoa bali kujiunga na jeshi na kwenda vitani.
Padri huyo aliendelea kufungisha ndoa kisiri ndipo mfalme akaamuru akamatwe na anyongwe. Miaka kadhaa badaaye Warumi wakaamua kuiteua siku hii kuadhimisha maisha ya mtetezi wa wapendanao.
Baadhi ya waumini wa Kanisa Katoliki jijini Mwanza Februari 13, 2023 wameiambia Nukta Habari (www.nukta.co.tz) kuwa ni muhimu kutembelea watu wanaohitaji faraja kama wafungwa, wagonjwa, yatima na waathirika wa dawa za kulevya ili kuonesha upendo ndani ya siku hii.
“Sijui hiki kitu kinatokea wapi, ila viongozi watufundishe siku ya wapendanao ni kwa ajili ya kuonyesha upendo wetu kwa wengine na wala si kwa ajili ya uzinifu…” amesema Mama Baraka Mkazi wa Wilaya ya Misungwi jijini Mwanza.
Mzee Ezekiel Kamwaga (81), mkazi wa kata ya Luchelele wilayani Nyamagana jijini hapa amesema kuwa utandawazi umebadilisha dhana ya siku ya wapendanao kuwa ya kufanya maovu.
“Viongozi wetu wa zamani walipoikubali siku hii walikuwa na maana nzuri tu na nakuahidi viongozi hawa wa sasa wakifumbia macho hali hii kizazi kijacho kitaiharibu kabisa siku ya wapendanao kutenda dhambi tu…” ameongeza Mzee Kamwaga.
Baadhi ya Watawa wameiambia Nukta Habari kuwa kukithiri kwa maovu ndani ya siku ya wapendanao kumeendelea kupoteza thamani ya siku hiyo na lengo la Kanisa Katoliki.
Sr. Anusiata Karoli amesema kuwa siku ya wapendanao sasa inatazamwa kuwa inatumia gharama kubwa kuipamba na inasababisha vurugu baina ya watu.
Katika kujibu baadhi ya hoja zilizotolewa na baadhi ya waumini wa Kikristo, Padri Titus Amigu kutoka Kanisa Katoliki la Martine De Pose lililopo wilayani Nyamagana amesema kuwa siku ya wapendanao itumike kudhihirisha upendo kwa familia, watoto na jamii kwa ujumla.
“Kanisa halina uwezo wa kumfunga mtu, kazi yetu ni kusema kutii ni jukumu la mwamini,” amesema Padre Amigu na kuongeza kuwa,
“Mwamini wetu ingemfaa afanye mambo matano ili kunufaika na siku hii, kwanza asahihishe nia ya mahusiano yake yasiwe ya tamaa ya mwili, pili vijana wajue lengo la mapenzi, tatu kujifunza maisha ya ndoa nne kuhimizana kupendana na mwisho siku hii itukumbushe upendo wa kweli.”