Huu ndio utamu wa kachumbari ya kabeji
- Siri ya kuandaa kachumbari tamu ya kabeji ipo kwenye namna unavyochanganya viungo vyake.
- Ili uweze kuifurahia kachumbari zaidi unaweza kuiweka katika jokofu na ukaitumia baada ya muda fulani.
Kabeji ni miongoni mwa mboga maarufu nchini Tanzania na maeneo mengine duniani ikitumika kama sehemu ya mlo au mlo kamili kwa baadhi ya watu waliopo katika programu ya kupunguza uzito.
Mboga hiyo yenye wingi wa virutubishi ikiwemo vitamin K, A na B9 hulimwa zaidi katika mikoa ya nyanda za juu yenye hali ya hewa ya ubaridi na mvua za kutosha, pamoja na baadhi ya maeneo ya nyanda za kati.
Mbali na kutumika zaidi kama mboga, kabeji linaweza pia kutumika kama saladi au kachumbari tamu inayoweza kunogesha mlo wowote ikiwemo wali, pilau au biryani.
Siri ya kuandaa kachumbari tamu ya kabeji ipo kwenye namna unavyochanganya viungo vyake na Jiko point leo tupo hapa kukuelekeza hatua kwa hatua namna ya kuandaa.

Namna ya kuanza kuandaa kachumbari ya kabeji tamu
Anza kwa kununua kabeji lenye ukubwa unaopenda kisha toa majani ya juu ambayo mara nyingi huwa yamechafuka au kuliwa na wadudu.
Ukimaliza osha kabeji kwa maji, baada ya hapo ligawe katikati na uanze kukata vipande vyembamba vyembamba au kukwangua na kifaa maalum.
Aina hiyo ya ukataji wa kabeji huifanya kachumbari iwe rahisi kutafunika na kuchanganyikana na viungo
Kama hupendi kabeji ikiwa mbichi kabisa, unaweza kuipasha moto kwa dakikan moja hadi mbili bila kuweka maji wala mafuta ili ilainike kidogo kabla ya kuichanganya na viungo vingine.
Baada ya hapo, ili kujipata utamu wa kujilamba chukua viungo vyako changanyia ikiwemo karoti zilizosagwa na hoho za rangi tofauti zilizokatwa nyembamba huleta muonekano mzuri wa rangi
Ongeza vitunguu maji na tango vilivyokatwa vyembamba na kusafishwa kwa maji ya chumvi ili kuondoa ukali na kuacha ladha tamu,
Pia ongezea ndimu ya maji au siki (Vinegar) ambayo hufanya kachumbari iwe na ladha ya ukali wa wastani inayochangamsha mdomoni pamoja na kuongezea chumvi.
Unaweza pia kuongeza pilipili manga, kiasi kidogo cha tangawizi, punje moja ya kitunguu swaumu ili kuongeza ladha zaidi.
Ili uweze kuifurahia kachumbari zaidi unaweza kuiweka katika jokofu na ukaitumia baada ya muda fulani.