Fedha za Uviko-19 kununua magari 195 ya wagonjwa Tanzania
- Ni kati ya Sh1.3 trilioni zilizotolewa na IMF kupambana na Uviko-19.
- Halmashauri zote nchini kupata magari hayo.
- Wabunge waanza kuyaomba kabla hayajanunuliwa.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imepanga kununua magari ya wagonjwa 195 kutoka katika fedha zilizotolewa na Shirika la Fedha Duniani (IMF) kukabiliana na athari za kijamii na kiuchumi za Uviko-19 ili kurahisisha huduma katika vituo vya afya.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi Dk Festo Dugange amesema hayo bungeni jijini Dodoma leo (Juni 9, 2022) wakati wa kipindi cha maswali na majibu huku akisisitiza kuwa baada ya ununuzi wa magari hayo halmashauri ndiyo zitafanya tathimini ya uhitaji wa magari ya wagonjwa kupelekwa katika vituo cha afya.
“Ni maamuzi ya halmashauri kuona kipaumbele kwa wakati huo, gari hilo litakwenda katika kituo cha afya au kwenye hospitali ya halmashauri,” amesema Dk Dugange
Huenda idadi hiyo ya magari yanayotarajiwa kununuliwa ikaongezeka kwa kuwa Serikali ina mpango wa kushirikiana na Shirika la Watoto Duniani (UNICEF) katika ununuzi wa magari hayo.
Soma zaidi:
Tanzania ina jumla ya halmashauri 184 ambapo katika mpango huo wa ununuzi wa magari hayo yanayotumiwa kubeba wagonjwa hasa wakati wa dharura, ugawaji utazingatia maeneo yenye uhitaji mkubwa.
Septemba 2021, Shirika la Fedha Duniani (IMF) liliidhinisha kuipatia Tanzania mkopo wa dharura wa Dola za Marekani milioni 567.25 (Sh1.3 trilioni) kwa ajili ya kukabiliana na athari za ugonjwa wa Corona (Uviko-19).
Fedha hizo zilizotolewa na IMF zinatumika ndani ya miezi tisa kuimarisha sekta elimu, maji na afya kwa kuongeza kasi ya utoaji chanjo ya Uviko-19, uboreshaji wa sera za fedha ili kuendana na hali ya wakati huu na kuinua sekta isiyo rasmi ambayo imeajiri Watanzania wengi.
Wabunge wayaomba magari hayo
Baadhi ya wabunge wameomba Serikali kupeleka magari hayo kwenye majimbo wanayotokea kutokana na uwepo wa uhaba wa magari ya wagonjwa.
“Kutokana na ukubwa na upekee wa hospitali ya Kawe iliyokuwa Mabwepande, hamdhani kwamba (Serikali) jimbo la kawe linatakiwa kupata gari kwa upekee?,” ameuliza Halima Mdee, Mbunge wa Viti Maalumu
Naye Boniphace Butondo, Mbunge wa Kishapu amesema “ninaomba kuletewa gari na lipelekwe katika tarafa ya Mondo ambayo itaongeza uwepo wa magari kwenye tarafa hiyo.”