EABC yataka mfanano tozo vipimo vya Corona Afrika Mashariki

January 11, 2021 11:04 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Yaziomba nchi za jumuiya hiyo kuwa na tozo nafuu na zinazofanana.
  • Yasema itasaidia kuongeza kasi ya biashara ya mipakani.
  • Pia yashauri muda wa kukaa karantini nao ufanane kwa nchi zote. 

Dar es Salaam. Baraza la Biashara la Afrika Mashariki (EABC) limeziomba nchi wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kuweka viwango vinavyolingana vya tozo za vipimo vya ugonjwa wa Corona ili kupunguza gharama za kufanya biashara na kuchochea ushirikiano wa kibiashara baina ya nchi hizo. 

Kwa sasa, tahadhari za kiafya na vipimo vya COVID-19 vinatozwa kwa gharama tofauti miongoni mwa nchi wanachama, jambo linaloibua changamoto kwa wafanyabiashara wanaoendesha shughuli zao katika mataifa hayo. 

Mathalan, nchi za Tanzania na Burundi zinatoza Dola za Marekani 100 (Sh230,000) kwa raia wake na wale wa kigeni wanaosafiri nje ya nchi kupata kipimo hicho ikiwa wanahitaji kupata cheti cha COVID-19. 

Mkurugenzi Mtendaji wa EABC, Dk Peter Mathuki ameeleza katika taarifa yake iliyotolewa leo Januari 11, 2020 kuwa kutofautiana huko kwa tozo kunaathiri ukuaji wa biashara na mshikamano wa jumuiya hiyo yenye nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini.

“Sektretarieti ya EAC iongeze kasi ya ushirikiano na mshikamano wa kikanda hasa katika tahadhari za COVID-19 kwa ajili ya ukuaji wa uchumi wa jumuiya ya EAC,” amesema Dk Mathuki. 


Zinazohusiana


Aidha, amewaomba viongozi wa jumuiya hiyo kuanzisha muda unaofanana wa kukaa karantini kwa wasafiri na kuongeza kasi ya utoaji majibu ya vipimo ya COVID-19 ili kupunguza muda wanaotumia wasafiri kupata majibu. 

Amesema changamoto hizo zisipopatiwa ufumbuzi wa pamoja, zitaendelea kuathiri biashara inayofanyika mipakani katika jumuiya hiyo na kuzorotesha ustawi wa wananchi wake. 

Januari 7, 2020, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ya Tanzania ilitoa toleo jipya la mwongozo wa upimaji wa ugonjwa Corona kwa watu wanaosafiri nje ya nchi kutokana na kuongezeka kwa watu wanaoambukizwa ugonjwa huo duniani. 

Mwongozo huo wa pili ulioanza kutumika Januari 4 mwaka huu umeibua mjadala mpana kwenye jamii hasa kiwango cha tozo cha Dola za Marekani 100 ambacho kila anayesafiri nchi za nje anatakiwa kulipa ili upate kipimo cha COVID-19.

Kiwango hicho cha tozo kimeongezeka kutoka Sh40,000 ya awali ambayo ilikuwa ikitumika kwa wazawa na Sh60,000 kwa wageni. 

Baadhi ya watu kwenye mitandao wamesema gharama hizo ni kubwa na watu wengi watashindwa kuzimudu hasa wale wanaosafiri mara kwa mara. 

Hata hivyo, waziri wa wizara hiyo, Dk Dorothy Gwajima katika mwongozo huo ameeleza kuwa kupanda kwa tozo hiyo kunatokana na mabadiliko ya teknolojia katika upimaji ambapo baadhi ya nchi zimeomba kuongeza kipimo cha “IgM Antibody” sanjari na PCR na kuongezeka kwa mahitaji ya kuchukulia sampuli, hivyo kupandisha gharama za vipimo. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW