Dk Mabula: Wasakwe kokote walipo warudi shuleni
Mbunge wa Jimbo la Ilemela Dk Angeline Mabula akikagua ujenzi wa bweni la wasichana katika Shule ya Sekondari Igogwe. Mbunge huyo yupo jimboni kwake akikagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Picha | Mariam John.
- Ni wanafunzi saba ambao hawajaripoti kidato cha kwanza Shule ya Sekondari Igogwe.
- Waziri wa Ardhi aagizwa wasakwe wao na wazazi wao.
Mwanza. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk Angeline Mabula amewaagiza watendaji kuhakikisha wanawatafuta wanafunzi saba ambao bado hawajaripoti kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Igogwe wilayani Ilemela mkoani Mwanza.
Waziri Mabula ametoa agizo hilo alipofanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya kupunguza umasikini (TPRPIV- OPEC) jimboni kwake na kueleza kuwa zipo taarifa za baadhi ya wanafunzi hao kutoroka nyumbani na wengine kuolewa.
“Hao watoto saba na wazazi wao lazima wapatikane kama kushitakiwa anashitakiwa mzazi na mtoto, haiwezekani Rais anatoa fedha ya kutosha ya kuweka miundombinu Sh516 milioni kwa Kata moja, lakini wao hawaripoti shule,” ameeleza Dk Mabula.
Ameeleza kuwa katika shule hiyo, ilipangiwa wanafunzi 167 wa kidato cha kwanza kwa mwaka wa masomo wa 2023, kati yao 160 wameripoti shuleni na waliobaki hawajaripoti na sababu zikielezwa kuwa baadhi yao wameolewa na wengine walitoroka nyumbani.
Amesema suala la shule sio la kuchukulia mzaha hasa kipindi hiki ambapo Serikali inaboresha miundombinu ya shule.
Pia ameeleza kuwa wanataka watoto wote waendelee na masomo hawataki kuona mtoto anaishia darasa la saba.
“Kwenye elimu hatutaki mchezo tunachohitaji watoto wote wasome, niwapongeze kuwa ni kiwago kidogo cha wanafunzi ambao hawajaripoti lakini taarifa zao siyo nzuri kwa sababu wengine wameolewa, wengine wamekimbia hapana lazima wapatikane na bahati nzuri Rais aliisha ridhia mtoto akipata ujauzito anapata fursa ya kuendelea na masomo watafutwe waendelee na shule,” ameeleza waziri huyo.
Awali Mkuu wa shule ya sekondari Igogwe Atanas Manyika amesema shule hiyo kwa mwaka mpya wa masomo 2023 ilipangiwa wanafunzi 167.
“Hatuna taarifa rasmi sana lakini zilizopo zinasemekana kuwa wengine wameolewa na wengine walitoroka baada ya kumaliza darasa la saba ,tayari tumeanza kuchukua hatua ikiwemo kupeleka taarifa zao ngazi za juu,” amesema Manyika
Mbali na ziara hiyo pia Waziri huyo amekagua ujenzi wa barabara ya Kahama kuelekea Shibula, barabara ya Igombe mwaloni, zahanati ya Mihama pamoja na eneo la ujenzi wa zahanati mpya katika kata ya Kitangiri.
Latest