Corona: Chanjo ya Abdala haibagui jinsia
- Hakuna chanjo inayoitwa Abdallah bali ipo inayoitwa Abdala kutoka nchini Cuba.
- Hakuna taarifa zozote zinazoonyesha kuwa chanjo ya Abdala inawafaa wanawake.
Dar es Salaam. Habari inayosambaa katika makundi ya WhatsApp nchini Tanzania ikiwa na picha za chupa za chanjo ya aina ya Abdala ni ya kutiliwa mashaka kwa sababu habari hiyo ya uzushi imesema inafaa zaidi wanawake.
Picha hiyo imeambatana na maelezo katika lugha ya Kiswahili yanayodai “Hii Chanjo ya Abdallah ndo yawafaa Wanawake”.
Ukweli uko wapi?
Habari hiyo ni ya kutilia mashaka kwa sababu ina upotoshaji ndani yake hakuna chanjo inayoitwa Abdallah kama ilivyoelezwa na mtoa taarifa bali kuna chanjo aina ya Abdala ambayo imetengenezwa nchini Cuba.
Chanjo ya Abdala ambayo imethibitishwa hivi karibuni na Cuba ikiwa katika awamu ya tatu ya majaribio yake kuwa na ufanisi wa asilimia 92.3 kama mtu atafanikiwa kupata dozi zote tatu za chanjo hiyo.
Chanjo hiyo imetengenezwa nchini Cuba na taasisi mbili za Center for Genetic Engineering and Biotechnology of Cuba ambapo Februari 1, 2021 ilianza kufanyiwa majaribio ya awamu ya pili.
Chanjo hiyo ni ya pili kutangazwa nchini humo baada ya Soberana 2, chanjo ambayo ufanisi wake ni asilimia 62 kwa dozi mbili tu kati ya tatu.
Chanjo zote mbili zinatarajiwa kuidhinishwa kwa matumizi ya dharura siku chache zijazo na mamlaka nchini humo.Cuba ambayo hadi Juni 23, 2021 imeripoti kesi 170,854 za Corona na vifo 1,180 imekataa kuagiza chanjo za nje badala yake itatumia chanjo ambazo imetengeneza yenyewe.
Inafaa wanawake pekee?
Tofauti na maelezo ya uzushi uliotolewa katika picha hiyo hapo juu, maelezo yaliyotelewa na watengenezaji wa chanjo hiyo ni kuwa chanjo hiyo inalenga watu wa jinsi zote .
Hata hivyo, chanzo zote za Corona ambazo zimeidhinishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) hakuna hata moja ambayo inabagua wanawake au wanaume. Kwa hiyo madai ya anayesambaza habari hiyo hayana mashiko kwa sababu chanjo za Corona hazibagui jinsia fulani.
Latest