Chaneli ya utalii Tanzania yatakiwa kwenda kidijitali

March 16, 2022 7:04 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Wanayoiendesha watakiwa kuongeza wigo wa kuwafikia watu.
  • Watakiwa kuwahudumia watumiaji wa mitandao ya kijamii.

Dar es Salaam. Licha ya chaneli ya utalii Tanzania kuwa sehemu muhimu ya kutangaza vivutio vya utalii nchini, wadau wanayoiendesha wametakiwa kuongeza ubunifu katika utengenezaji wa vipindi ili viwafikie na watumiaji wa mitandao ya kijamii.

Chaneli hiyo (Tanzania Safari Channel) inasimamiwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na kupatikana katika ving’amuzi mbalimbali kikiwemo cha Startimes.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Balozi, Dk Pindi Chana amewataka wadau wa chaneli ya utalii kuhakikisha wanatanua wigo wa vipindi vya utalii viweze kuonekana katika mitandao ya kijamii. 

Waziri Dkt. Pindi ametoa agizo hilo jijini Dodoma Machi 15, 2022 wakati akizungumza na wadau wa chaneli hiyo na manaibu mawaziri kwa lengo la kujadili mikakati na maboresho ya channeli hiyo ili kufanikisha malengo ya kuanzishwa kwake.

“Moja ya mapendekezo ilikuwa ni kuhakikisha inapatikana katika visimbuzi vyote  na majukwaa mengine nchini  na hapa kuna wataalamu mtatuambia  hii haitoshi tuweke na kwenye simu, mitandao ya kijamii  ndiyo maana kikao cha leo kina wabobezi hivyo ni lazima tufikiri nje ya boksi  kama tunazungumzia utalii siyo lazima mtu afike nyumbani ndipo awashe luninga yake zionekane hata katika vyombo vya usafiri,” amesema Dk Pindi.

Amesema chaneli hiyo inapaswa kuwa endelevu na vipindi vinavyoandaliwa  viwe vyenye  ushawishi kwa wananchi kuvutiwa kutembelea vivutio vilivyopo nchini hata mataifa ya nje kutembelea vivutio hivyo.


Zinazohusiana:


Aidha, amesema masuala ya utalii ni mtambuka yanayoshirikisha sekta mbalimbali kama sekta ya utalii, sekta ya uchukuzi, sekta ya habari na mawasiliano na  sekta ya fedha hivyo kama wasimamizi wa sera katika wizara husika ipo haja ya kuifahamu chaneli hiyo, lengo la kuanzishwa na umuhimu wake kwa sekta ya utaliii na uchumi kwa nchi.

Akieleza mapendekezo yaliyofikiwa na wataalamu wa sekta hiyo mara baada ya kikao cha Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, Kaspar Mmuya amesema maazimio yaliyofikiwa ni pamoja na Mawaziri kuendelea kupewa nafasi ya kuwasilisha mawazo yao, wanaochangia kwa kujitolea kuwezesha chaneli watambuliwe  na kila taasisi kuweka utaratibu utakaowezesha uchangiaji wa Safari Chaneli.

Mkurugenzi wa TBC, Dk Ayoub Ryoba amesema tangu kuanzishwa kwa chaneli hiyo wamefanikiwa kununua na kufunga mitambo ya kidigitali, kurusha matangazo kote duniani, kurushwa vipindi vyake kupitia visimbuzi vyote nchini, kuboresha vifaa, kutoa elimu ya utalii kwa Watanzania kuptia vivutio vya kiutamaduni, hifadhi za wanyama na utalii wa Ikolojia.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW