Chadema kuanza wiki ya maandamano nchi nzima
- Maandamano hayo yatafanyika Aprili 22 hadi 30 mwaka huu.
- Wanachama wake katika maeneo mengine duniani kuandamana katika nchi zao.
Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimetangaza kuanza kwa wiki ya maandamano yatakayofanyika kuanzia tarehe 22 hadi 30 Aprili 2024 katika makao makuu ya chama hicho nchi nzima.
Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe aliyekuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 6, 2024 mkoani Mtwara amesema uamuzi huo umetokana na Serikali kupuuzia maandano yaliyopita na hali ngumu ya maisha iliyopo nchini.
“Kwa vile Serikali imekataa mabadiliko ambayo Watanzania wameyataka kwa nia za mazungumzo na maridhiano sasa Watanzania watayapata mabadiliko hayo kwa njia ya nguvu ya umma na njia nyingine za shinikizo kama maandamano, migomo na njia nyingine,” amesema Mbowe.
Aidha kiongozi huyo amewataka wananchama wa Chadema waliopo katika maeneo mengine duniani kuandamana katika miji yao ili kufikisha ujumbe wa hali iliyopo nchini Tanzania.
Maamuzi hayo ya wiki ya maandamano yanayofanyika na Chadema ni sehemu ya azimio lilioandaliwa na kamati kuu ya chama hicho iliyokutana kwa kuanzia Machi 4 hadi Machi 6 mkoani Mtwara.