CCM yarejesha wagombea wote wa udiwani kwenye kura za maoni

August 1, 2025 10:10 am · Fatuma Hussein
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni kutokana na malalamiko ya wanachama na wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini waliopinga kuenguliwa kwa watia nia wao.

Dar es Salaam. Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imetoa uamuzi wa kurejesha wagombea wote wa nafasi ya udiwani katika kata mbalimbali nchini kwenye mchakato wa kura za maoni, zitakazofanyika Jumatatu, Agosti 4, 2025.

Hatua hii inafuatia malalamiko ya wanachama na wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini waliopinga kuenguliwa kwa watia nia wao.

Mathalani siku za hivi karibuni zilionekana video kwenye mitandao ya kijamii za wanachama wa CCM wakishinikiza wagombea waliokatwa warejeshwe ikiwemo wakazi wa Kijiji cha Muze Kata ya Muze katika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa,

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Amos Makalla, uamuzi huo ulitokana na kikao cha sekretarieti kilichofanyika Alhamisi, Julai 31, 2025. 

Taarifa hiyo imeeleza kuwa wagombea wote waliokuwa kwenye orodha ya awali ya nafasi ya udiwani, pamoja na wale waliopitishwa na kamati za siasa za mikoa, wanapaswa kurejeshwa kwenye orodha rasmi ya kura za maoni bila kuondolewa.

Uamuzi huu unamaanisha mchakato huo sasa utakuwa wa wazi zaidi, ukitoa nafasi kwa wanachama wa CCM kufanya maamuzi yao moja kwa moja kupitia kura za maoni. 

“Wagombea wote waliopitishwa na Kamati za Siasa za Mikoa warejeshwe rasmi kwenye orodha ya kura za maoni. Vilevile, wagombea wote waliokuwemo kwenye orodha ya awali waliotumwa kwa makatibu wa mikoa waruhusiwe kushiriki kura hizo,” imeeleza taarifa hiyo.

Makalla amefafanua kuwa maelekezo hayo mapya yanabatilisha maagizo yote ya awali yaliyotolewa kuhusu uteuzi wa wagombea wa nafasi ya udiwani. 

Amesisitiza kuwa maagizo haya mapya ndiyo yanatakiwa kuzingatiwa na kutekelezwa kikamilifu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha haki, usawa na utulivu ndani ya chama kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Jumatano, Oktoba 29, 2025. 

Sekretarieti imehimiza utekelezaji wa maagizo hayo ufanyike mara moja bila kucheleweshwa, huku ukizingatia miongozo ya chama.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW