CCM yamteua Asha Hussein Salehe kuwania ubunge jimbo la Fuoni 

October 21, 2025 3:46 pm · Fatuma Hussein
Share
Tweet
Copy Link
  • Amechukua nafasi ya aliyekuwa mgombe ubunge katika jimbo hilo Abbas Ali Mwinyi kabla ya kukutwa na umauti.

Dar es Salaam. Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimemteua Asha Hussein Salehe kuwa mgombea wa ubunge katika jimbo la Fuoni, kufuatia kikao maalum cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho(CC).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Oktoba 21, 2025 na Katibu wa NEC-Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi imesema kuwa kikao hicho kilichofanyika jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Samia Suluhu Hassan kimeangazia ajenda mbalimbali za chama, ikiwemo uteuzi wa mgombea atakayewakilisha CCM katika uchaguzi mdogo wa ubunge utakaofanyika Desemba 30, 2025.

“Uteuzi huo umefanyika kwa kuzingatia Ibara ya 105 (7)(f) ya katiba ya CCM ya mwaka 1977, toleo la Mei, 2025 pamoja na kanuni ya 9 (2) ya kanuni za uteuzi wa wagombea uongozi katika vyombo vya Dola, toleo la Machi 2025,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

Uteuzi huo wa Asha Salehe unakuja zikiwa zimepita siku 26 baada ya kifo cha aliyekuwa mgombea wa jimbo hilo Abbas Ali Mwinyi.

Aidha, Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa imetoa pole kwa Makamu Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Zanzibar, Hussein Ali Mwinyi, kufuatia kifo cha kaka yake, Abbas Ali Mwinyi, kilichotokea Septemba 25, 2025.

Marehemu Abbas Mwinyi alikuwa mgombea wa kiti cha ubunge wa Jimbo la Fuoni kupitia CCM katika uchaguzi uliopita. 

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa CCM Taifa, Samia Suluhu Hassan, amesema chama kimepoteza kiongozi mahiri na mwanachama mwadilifu, huku akitoa pole kwa familia ya marehemu.

Hata hivyo, mgombea huyo wa kiti cha Urais kwa tiketi CCM pia amewapongeza waratibu wa kampeni za chama kote nchini kwa kujitolea na kuhakikisha kuwa CCM inaendelea kushinda kwa kishindo katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29 2025.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW