Badala ya kuonja maji kutambua kiwango cha chumvi, sasa wakulima wanatumia simu janja

January 28, 2021 6:28 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni kiwango cha chumvi kwenye maji yanayotumika katika kilimo cha mpunga.
  • Sasa hawatumii ulimi kupima chumvi lakini wanatumia programu maalum ya simu.
  • Ni wakulima wa Vietnam ambao wameanza kuongeza uzalishaji na mavuno. 

Dar es Salaam. Simu za mkononi zimekuwa mkombozi kwenye kilimo kuanzia Tanzania, Bolivia hadi Cambodia ambapo teknolojia ziwe za kuuza bidhaa au kutambua hali ya hewa zimesaidia wakulima na wavuvi kutambua msimu wa mavuno, uvuvi au upandaji mazao.  

Nchini Vietnam, wakulima wa mpunga wamekuwa wakipata changamoto ya kutambua ni vipi wanaweza kuongeza kiwango cha mavuno katika kilimo chao cha mfumo wa umwagiliaji. 

Thach Thi Than ni mkulima katika jimbo la Tra Vinh akihojiwa na redio ya Umoja wa Mataifa (UN) amesema “pindi maji yenye chumvi yanapoingia shambani, huathiri mpunga na hata kuua mpunga wote. 

“Mathalani msimu uliopita, shamba letu la mpunga liliharibika. Kwa kawaida tunapata magunia 16 ya mpunga kwa ekari moja lakini kwa sababu ya kiwango kikubwa cha chumvi kwenye maji tunapata magunia matano hadi sita. Kwa hiyo chumvi inatuathiri sana.” 

Hata hivyo, mambo yamebadilika, Mfuko wa Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (IFAD) umesaidia wakulima kuondokana na tabia ya kuonja maji ya umwagiliaji ili kutambua kiwango cha chumvi na badala yake sasa wanatumia teknolojia ya simu za mkononi ili kuongeza mavuno ya mpunga. 

IFAD kwa kushirikiana na kampuni ya RYNAN wamekuja na teknolojia ya kuweka kifaa maalum shambani na kusoma kiwango cha chumvi na matokeo yake kuonyeshwa kwenye simu ya kiganjani.

Meneja wa mradi wa IFAD, Huynh Nghia Tho anasema “kila dakika 15, sampuli ya maji inachukuliwa na taarifa zinapelekwa kwenye kituo cha operesheni, zinachambuliwa kiwango cha chumvi, uwezo wa maji kukabili na hata kiwango cha mawimbi ya maji. 

“Hatimaye wakulima wanapatiwa taarifa kupitia app (programu) iliyoko kwenye simu.” 


Zinazohusiana: 


Kwa mkulima Than, haya ni mapinduzi ya kilimo huku akiambia redio ya Umoja wa Mtaifa kuwa “zamani, wazazi wetu walipotaka kutambua iwapo maji yana chumvi au la, waliyaonja ili hatimaye waamue kuyafungulia kwenye shamba au la. Lakini sasa tunaweza kusalia nyumbani na kuweza kupata taarifa za kiwango cha chumvi kwenye maji.” 

Kipimo hicho kinasaidia watu kupunguza hatari ya kufungulia maji ya chumvi kwenye mashamba yao ya mpunga na hivyo kuongeza uzalishaji. 

Miradi kama hiyo inatekelezwa wakati huu ambapo IFAD imetambua umuhimu wake na imezindua mpango wa Dola za Marekani milioni 500 (Sh1.2 trilioni) wa kusaidia wakulima kufuata kilimo cha kisasa na kinachohimili mabadiliko ya tabianchi unajulikana kama ASAP+.

Hivi sasa ni asilimia 1.7 ya fedha  kwenye mfuko wa mabadiliko ya tabianchi ndiyo zinafikia wakulima wadogo. 

Enable Notifications OK No thanks