Ahueni,maumivu zaidi: Bei ya mahindi yashuka Tanzania
- Bei ya zao hilo imeshuka kwa asilimia 20.7 katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
- Bei ya zao yaanza kupanda katika miezi ya hivi karibuni.
- Serikali yafungua milango wananchi kuuza mahindi popote.
Dar es Salaam. Ikiwa umepita mwezi mmoja tangu Serikali ya Tanzania itangaze kutoa Sh15 bilioni kununua mahindi ya wakulima, bei ya zao hilo imeshuka kwa asilimia 20.7 katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita unaoishia mwezi Agosti 2021.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa bungeni Septemba 2 mwaka huu alisema Serikali imeshatoa Sh15 bilioni kwa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) ili kununua mahindi kutoka kwa wakulima.
“Uzalishaji wa mahindi ni mkubwa lakini na sisi pia tumeimarisha hifadhi yetu ya Taifa ya chakula (NFRA) tumeipa fedha za kwenda kununua mahindi kwa bei ya kumuwezesha mkulima ili ajikimu hadi msimu ujao,” alisema Majaliwa.
Hatua hiyo ililenga kuwapa ahueni wakulima ambao wamekuwa na malalamiko ya kuwa na mahindi mengi yaliyokosa soko na hivyo kuwaweka katika hatari ya kupata hasara.
Licha ya Serikali kuanza kununua mahindi hayo, bei ya jumla ya mahindi kwa gunia la kilo 100 imeshuka hadi Sh44,811 katika mwaka ulioishia Agosti 2021 kutoka Sh56,560 iliyokuwa ikitumika mwaka ulioishi Agosti mwaka jana.
Hiyo ni kwa mujibu wa Ripoti ya Mapitio ya Uchumi kwa mwezi Septemba 2021 (Monthly Economic Review) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) iliyotolewa hivi karibuni.
Hiyo ina maana kuwa bei ya mahindi imeshuka kwa asilimia 20.7 au sawa na kusema wakulima waliouza mahindi mwezi Agosti wamepoteza Sh117,48 kwa kila gunia moja, fedha ambayo walikuwa wanaipata Agosti mwaka jana.
“Kushuka huku kwa bei kunachangiwa na usambazaji wa chakula wa kutosha sokoni kutokana na hali ya hewa nzuri katika msimu wa 2020/21,” imeeleza ripoti hiyo.
Licha ya bei ya mahindi kushuka kwa mwaka mmoja uliopita, matumaini ya kupanda kwa zao hilo yameanza kuonekana katika miezi ya hivi karibuni, jambo linaloweza kuwasaidia wakulima kufaidika la ongezeko la bei katika siku zijazo.
BoT inaeleza kuwa tangu mwezi Juni mwaka huu, bei ya zao hilo la chakula imekuwa ikipanda mfululizo hadi kufikia Sh44,811 mwezi Agosti mwaka huu.
Bei inaweza kuendelea kupanda ikizingatiwa kuwa Serikali kwa sasa inanua mahindi ya wakulima na imefungua milango kwa wakulima kuuza mahindi yao nje ya nchi ili kujipatia kipato.
Latest