Gharama, elimu ya kidigitali vikwazo vya ukuaji wa ‘Fintech’ Tanzania
- Zaidi ya watumiaji milioni 300 wamejisajili kutumia huduma za ujumuisha wa kifedha kwa njia nya kidigitali.
Dar es Salaam. Licha ya teknolojia ya kifedha (‘Fintech’) kuendelea kukua nchini Tanzania wadau wa sekta ya fedha wamebainisha vikwazo vinavyoweza kurudisha nyuma jitihada za ukuaji wa teknolojia hizo.
Fintech ni jumla ya teknolojia zote zinazotumika katika sekta ya kifedha, ikijumuisha benki, mifumo ya malipo na biashara za kielektroniki, ambazo hurahisisha upatikanaji wa huduma na usalama wa kifedha kwa watumiaji.
Kennedy Komba Mkurugenzi wa Ujumuishaji na Upanuzi wa Huduma za Kifedha kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT) aliyekuwa akizungumza leo Machi 26,2026 amesema Fintech inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo ukosefu wa elimu ya digitali.
“Vikwazo bado vipo, kama vile gharama kubwa ya intaneti, ukosefu wa elimu ya kidijitali na uhitaji wa bidhaa zinazozingatia mahitaji ya mteja..,” amesema Komba katika Jukwaa la Uwekezaji Afrika Mashariki (EAIF 2026) jijini Dar es Salaam.

Komba anafafanua kuwa changamoto nyingine inayoikabili sekta hiyo ni mgawanyiko wa kidijitali jambo ambalo linafanya maeneo ya mijini kukua kwa kasi kidijitali huku vijijini wakiendelea kukabiliana na vikwazo vinavyohusiana na kuunganishwa kwa mtandao na elimu ya kidigitali.
“Safari ya kuelekea uchumi wa kidigitali unaojumuisha kila mtu ni mbio za masafa marefu, si mbio za muda mfupi. Inahitaji ushirikiano endelevu, uundaji wa sera madhubuti, na ahadi ya kumweka mlaji katika kitovu cha kila kitu tunachofanya,” amesema Komba.
Pamoja na uwepo wa changamoto hizo Komba amebainisha kuwa mwaka 2025 zaidi ya watumiaji milioni 300 walijisajili kutumia huduma za kifedha kwa njia ya kidigitali huku upatikanaji wa huduma hiyo nchini ukifikia asilimia 95.

Huenda ongezeko hilo la matumizi ya Fintech yalichangiwa zaidi na kuongezeka kwa watumiaji wa intaneti nchini kutoka milioni 40 mwaka 2024 hadi miliioni 58.1 kama ilivyoainishwa katika ripoti ya robo ya nne ya mwaka 2025 inayotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Ufumbuzi watolewa
Ili kutatua changamoto hizo, Komba ameeleza kuwa BoT imeanzisha mfumo unaoruhusu kampuni changa za Fintech kufanya majaribio ya uvumbuzi wao chini ya uangalizi kabla ya kuingia sokoni rasmi.
Vilevile, inaendelea na utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Ujumuishi wa Kifedha (National Financial Inclusion Framework) unaolenga kutoa kipaumbele kwa masuluhisho ya kidijitali yanayomlenga mteja wa mwisho.

Awali akizungumza katika jukwaa hilo Mwenyekiti wa ‘Fintech’ Cynthia Ponera, amesema upatikanaji wa huduma za mikopo na akiba ni msingi wa maendeleo jumuishi hasa wakati ambao mafanikio ya sekta hiyo yanategemea mshikamano wa ubunifu, uthabiti pamoja na uwepo wa mifumo rafiki ya kisheria.
Latest