Polisi yatoa miezi miwili wananchi kusalimisha silaha haramu kwa hiari
- Silaha hizo zinatakiwa kuwasilishwa kuanzia Septemba 1 hadi Oktoba 31, 2025.
- Watakaowasilisha baada ya muda huo kuchukuliwa hatua.
Arusha. Jeshi la Polisi Tanzania limewataka wananchi wanaomiliki silaha kinyume cha utaratibu kuzisalimisha kwa hiyari kuanzia Septemba 1 hadi Oktoba 31, 2025.
Kwa mujibu wa Jeshi la Polisi wananchi watakaowasilisha silaha hizo ndani ya muda tajwa hawatachukuliwa hatua za kisheria.
Taarifa ya David Misime, Msemaji wa Jeshi la Polisi iliyotolewa leo Septemba 1, 2025 imebainisha kuwa msamaha huo ni kwa wananchi watakaowasilisha kwa hiari katika muda uliopangwa na baada ya hapo watachukuliwa hatua.
“Mtu yeyote atakayepatikana na silaha baada ya kipindi cha msamaha yaani baada ya Mwezi Septemba na Oktoba, 2025 atakamatwa na kuchukuliwa hatua zingine za kisheria,” imesema taarifa ya Misime.
Zoezi hilo linalotarajia kufanyika kwa miezi miwili ni maagizo ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Innocent Bashungwa kwa mujibu wa Kifungu cha 66 cha Sheria ya Udhibiti wa Silaha na Risasi ya Mwaka 2015, Sura ya 223 na marejeo ya mwaka 2023.
Kupitia kifungu hicho wananchi wamepewa wito kuziwasilisha silaha hizo katika kituo chochote cha polisi nchini, Ofisi ya Serikali za Mitaa kwa Mtendaji Kata au Shehia kuanzia muda wa saa mbili asubuhi hadi saa kumi jioni,
Kwa wale ambao ndugu zao walikuwa wanamiliki silaha kihalali na wamefariki wanatakiwa kuzisalimisha silaha hizo kulingana na masharti yaliyotajwa.
Aidha, Jeshi la Polisi limewaonya wamiliki binafsi wa silaha zikiwemo kampuni binafsi za ulinzi ambazo zimekuwa zikiazima au kuazimisha silaha kutoka au kwenda kwa watu wengine waache tabia hiyo mara moja kwa sababu ni kosa la jinai.
“Kama kuna silaha ambazo zinatumika isivyo halali zirejeshwe kwa wamiliki au zisalimishwe katika vituo vya Polisi katika kipindi hiki cha msamaha uliotolewa na Serikali,” imesisitiza taarifa ya Misime.
Silaha nyingine zinazotakiwa kusalimishwa ni zile zilizokuwa zinamilikiwa kihalali hapo awali na Kampuni binafsi za ulinzi ambazo zimesitisha kutoa huduma za ulinzi na silaha walizokuwa wanamiliki zikarithiwa na kampuni nyingine bila kufuata utaratibu wa kisheria.
Pamoja na hayo, wamiliki wote wa silaha wametakiwa kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya matumizi mabaya na utunzaji mbaya wa silaha huku wakizingatia Sheria na Kanuni na yeyote atakayekiuka, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ikiwa ni pamoja na kufutiwa Leseni.