Msako wanaomiliki silaha isivyo halali kuanza kesho
- Baada ya tarehe ya mwisho kusalimisha silaha hizo kuisha leo.
- Watakaokutwa nazo kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
Mwanza. Jeshi la Polisi mkoani Mwanza limesema kuanzia kesho litaanza msako wa silaha zinazomilikiwa isivyo halali huku likipokea silaha tano zilizosalimishwa na watu katika vituo vya polisi.
Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, Ramadhani Ng’anzi amesema kati ya silaha hizo tatu ni kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, moja wilayani Magu na iliyobaki imesalimishwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema.
Kusalimishwa kwa silaha hizo kunatokana na agizo la Serikali la hivi karibuni la kuwataka watu wote wanaomiliki silaha isivyo halali kuziwasilishwa katika vituo vya polisi au ofisi wa watendaji kata kabla hawajachukuliwa hatua za kisheria.
“Waziri (wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene) alitoa tangazo hilo mwezi mmoja uliopita kuwa wananchi wote wanaomiliki silaha kinyume cha sheria wazisalimishe kwenye ofisi na vituo mbalimbali vya serikali vilivyokaribu nao kabla msako haujaanza kufanyika, tunashukru wananchi wamejitokeza na Mwanza tumepokea silaha tano,” amesema Kamanda Ng’anzi
Kamanda huyo amesema bado wanaendelea kupokea silaha hizo hadi leo saa 6 usiku, hivyo wananchi wote ambao wanamiliki silaha kinyume cha sheria ofisi za serikali ziko wazi.
“Nitoe wito kwa wakazi wa Mkoa wa Mwanza ambao wanazimiliki isivyo halali wasalimishe katika vituo vya polisi, watendaji kata, watu wa serikali za mitaa. Wasipofanya hivyo hatua kali,” amesema kamanda huyo.
Amesema kuanzia kesho watapita nyumba kwa nyumba kuzisaka silaha zote ambavyo zinamilikiwa isivyo halali na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa watakaokamatwa nazo.
Silaha hizo ambazo hazimilikiwi isivyo halali zimekuwa zikitumika katika matukio mbalimbali ya uhalifu ikiwemo ujambazaji, unyang’anyi na hivyo kusababisha hasara kwa watu za mali na hata vifo.
Vitendo hivyo, uiongezea Serikali kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zake.
Latest
