HESLB yaongeza muda wa kuwasilisha maombi ya mikopo
- Ni kwa lengo la kuwapa fursa wanafunzi ambao hawakuweza kuwasilisha maombi yao kwa wakati waweze kuwasilisha.
Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu Tanzania (HESLB) imeongeza muda wa kuwasilisha maombi ya mikopo kwa mwaka wa masomo 2025/2026 kutoka Agosti 31 hadi Septemba 14, 2025.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na bodi muda huo umeongezwa ili kuwapa fursa wanafunzi ambao hawakuwasilisha maombi yao kwa wakati kuwasilisha.
Bodi ilianza kupokea maombi ya mikopo ya wanafunzi kwa njia ya mtandao kuanzia Juni 15, 2025, hadi na ilipangwa Agosti 31 kuwa tamati.
Kwa mujibu wa HESLB hadi Agosti 31, jumla ya maombi 157,309 yamepokelewa, ikiwa ongezeko la asilimia 5 ikilinganishwa na maombi 150,530 yaliyokuwa yamepokelewa mwaka jana.
“Aidha, maombi 960 ya ‘Samia Scholarship’ yamepokelewa, ikilinganishwa na 742 mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la asilimia 29,” imeeleza taarifa hiyo.
Hata hivyo, HESLB imesisitiza kuwa hakutakuwa na muda mwingine wa nyongeza baada ya tarehe 14 Septemba, 2025, hivyo waombaji wanatakiwa kukamilisha maombi yao ndani ya muda huo.