INEC yawarejesha wagombea ubunge, udiwani wanne, tisa waachwa
- Wabunge, madiwani waliorejeshwa waruhusiwa kuendelea na mchakato wa uchaguzi.
Arusha. Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imewarejesha wagombea wanne wa udiwani na ubunge waliokata rufaa ya uteuzi wa kuwania nafasi hizo katika majimbo yao.
Wagombea hao walikata rufaa kwa mujibu wa Kifungu cha 53(6) na 65(7) vya Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 vikisomwa pamoja na kanuni ya 29(1) ya Kanuni za Uchaguzi wa Rais na Wabunge na Madiwani za Mwaka 2025.
Vifungu hivyo vinabainisha kuwa rufaa inatakiwa kukatwa ndani ya saa 24 tangu aumuzi ulipotolewa.
Taarifa ya Mkurugenzi wa Uchaguzi wa INEC, Ramadhani Kailima, iliyotolewa jana Agosti 31, 2025 Jijini Dodoma, inabainisha kuwa kati ya rufaa 33 zilizopokelewa 13 zilifanyiwa maamuzi ambapo nne zilikubaliwa na tisa kutupiliwa mbali.
“Zifuatazo ni rufaa mbili za wagombea ubunge zilizokubaliwa, ndugu Ezekiel Gabriel Katabi mgombea ubunge Jimbo la Muhambwe kupitia Chama cha CHAUMMA dhidi ya msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Muhambwe na ndugu Athuman Issah Henku mgombea ubunge Jimbo la Ikungi Mashariki kupitia Chama cha CUF dhidi ya Ndugu Thomas Mgongo Kitima mgombea ubunge kupitia Chama cha Mapinduzi,” imesema taarifa ya INEC
Kwa upande wa udiwani walioshinda ni Yasini Mazoea Bakiri mgombea udiwani Kata ya Mlingula na Alex Tresiford Nachingulu mgombea udiwani Kata ya Mwena wotw wakitokea Jimbo la Ndanda kupitia Chama cha ACT-Wazalendo.
Rufaa zilizokataliwa
INEC imebainisha kuwa imezitupilia mbali rufaa tisa kati ya 13 zilizopokelewa ikiwemo ya Msowoya Goodluck mgombea ubunge Jimbo la Kilombero kupitia Chama cha ACT-Wazalendo dhidi ya Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Kilombero.
Nyingine ni rufaa ya Innocent Siriwa mgombea ubunge Jimbo la Kibamba kupitia Chama cha ADC,David January Mhanga mgombea ubunge Jimbo la Mkuranga kupitia Chauma , Christina Mbise mgombea ubunge Jimbo la Ubungo kupitia ADC, Cecil Akili mgombea ubunge Jimbo la Ndanda kupitia ACT-Wazalendo na Mneke Saidi mgombea ubunge Jimbo la Newala Vijijini kupitia CUF.
Aidha, taarifa ya INEC imesema wagombea sita wa ubunge ambao rufaa zao zimekataliwa ni Msowoya Gelard Goodluck mgombea ubunge Jimbo la Kilombero kupitia Chama cha ACT- Wazalendo dhidi ya Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Kilombero;
Kwa upande wa udiwani, ameeleza kuwa INEC imekataa rufaa tatu ikiwemo ya Abisai Hankungwe mgombea udiwani Kata ya Mabatini
Jimbo la Mbeya Mjini kupitia Chama cha Chaumma, Mwajuma Hamidu Tito mgombea udiwani Kata ya Nanganga Jimbo la Ndanda kupitia Chama cha CUF na ya Jacob Jaston Mdolo mgombea udiwani Kata ya Ilolo Jimbo la Vwawa kupitia CCM.
Amesisitiza kuwa uamuzi huu ni sehemu ya kuhakikisha uchaguzi mkuu unafanyika kwa uwazi, haki na kwa mujibu wa sheria za nchi.
“Tunaendelea kusimamia mchakato huu kwa misingi ya katiba na sheria, ili wagombea wote wapate haki sawa,” amesema Kailima.