‘Dogo Janja’ aibuka kidedea kura za maoni udiwani, Kata ya Ngarenaro
- Apata kura 76 za wajumbe kati ya kura 138, amshinda aliyekuwa diwani wa kata hiyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii ya Jiji la Arusha, Isaya Doita aliyepata kura 60.
Dar es Salaam. Msanii wa muziki wa Bongofleva, Abdulaziz Abubakar maarufu kwa jina la Dogo Janja ameibuka kidedea katika kura za maoni za Chama Cha Mapinduzi (CCM) akigombea nafasi ya udiwani wa Kata ya Ngarenaro, jijini Arusha.
Katika mchujo huo uliofanyika leo Agosti 4, 2025 kote nchini kwa ajili ya kupatikana kwa wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge kupitia CCM, Dogo Janja amepata kura 76 kati ya kura halali 138, akimshinda aliyekuwa diwani wa kata hiyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii ya Jiji la Arusha, Isaya Doita aliyepata kura 60.
Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo hayo, msimamizi wa uchaguzi wa chama hicho, Sophia Islam, amesema mchakato uliendeshwa kwa amani huku wanachama wakijitokeza kwa wingi kushiriki katika maamuzi ya ndani ya chama.
Ushindi wa Dogo Janja unakuja katika kipindi ambacho mijadala mizito imeibuka kwenye majukwaa mbalimbali ya mitandao ya kijamii kuhusu ushiriki wa wasanii na watu maarufu katika siasa, hasa katika kipindi hiki kuelekea Uchaguzi Mkuu 2025.
Wapo wanaohoji uwezo wa wasanii hao kuongoza jamii wakihusisha maisha yao ya kisanii na maadili ya uongozi, huku wengine wakieleza kuwa ni fursa ya kuwa na wawakilishi wanaowafikia watu wengi na kuhamasisha ushiriki wa vijana kwenye siasa.
Itakumbukwa kuwa hivi karibuni msanii maarufu wa Bongo Fleva na mchekeshaji, Clayton Chipando maarufu kama Baba Levo, naye alipenya katika hatua ya awali ya uteuzi kwa nafasi ya ubunge wa Kigoma Mjini kupitia CCM, baada ya jina lake kupitishwa na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho.
Dogo Janja sasa atasubiri hatua zinazofuata ndani ya chama hicho iwapo jina lake litaingia katika orodha ya mwisho ya wagombea wa nafasi ya udiwani katika Uchaguzi Mkuu 2025.