Baada ya Hidaya TMA yaonya uwepo wa kimbunga IALY
- Kitaikumba Madagascar na visiwa vya Shelisheli kwa siku nne zijazo.
- TMA yatoa angalizo kwa watumiaji Bahari ya Hindi.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari juu ya uwepo wa kimbunga “IALY” katika Bahari ya Hindi kaskazini mwa kisiwa cha Madagascar kinachoweza kusababisha upepo mkali na mawimbi makubwa.
TMA imetoa taarifa hiyo leo Mei 17, 2024 saa sita mchana ambapo imesema kimbunga hicho hakitakuwa na athari za moja kwa moja na kitakuwa katika maeneo ya Madagascar na visiwa vya Shelisheli kwa siku nne zijazo kabla ya kuanza kupungua nguvu.
“Kutokana na umbali kutoka nchini, kimbunga hicho hakitarajiwi kuwa na athari za moja kwa moja katika kusababisha ongezeko la mvua nchini. Hata hivyo vipindi vya upepo mkali na mawimbi makubwa vinaweza kujitokeza katika Bahari ya Hindi,” imesema taarifa ya TMA.
Taarifa za ujio wa kimbunga IALY zinakuja ikiwa ni siku15 tangu mamlaka hiyo itangaze ujio wa kimbunga Hidaya kilichokikumba mikoa ya kusini pamoja na pwani ya Bahari ya Hindi.
Soma zaidi:Kimbunga Hidaya chawatesa wavuvi nane baharini Dar es Salaam
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliyekuwa akizungumza Bungeni Dodoma mei 9, mwaka huu kimbunga hicho kilichomalizika Mei 4 kimesababisha vifo vya watu 10 pamoja na uharibifu wa miundombinu mingine.
Majaliwa ameutaja uharibifu huo kuwa ni pamoja na shule, barabara, kusimama kwa shughuli za uchumi, uharibifu wa chakula na madhara ya kisaikolojia.
Aidha, TMA imesema inaendelea kufuatilia mwenendo wa kimbunga hicho na athari zake kwa mifumo ya hali ya hewa hapa nchini na itaendelea kutoa taarifa kila inapobidi.
Pia imewataka watumiaji wa bahari na wananchi kwa ujumla kuendelea kufuatilia na kuzingatia taarifa za utabiri kutoka mamlaka hiyo pamoja na kupata ushauri na miongozo ya wataalamu wa kisekta.