Gazeti la Tanzania Daima lafutiwa leseni
- Serikali yasema limekiuka sheria za Tanzania na maadili ya vyombo vya habari.
- Yasema limeonywa zaidi ya mara 10 na wachapishaji wake wameomba msamaha mara mbili.
- Mhariri wa gazeti hilo asema wanajadili hatua za kuchukua baada ya kufutiwa leseni.
Dar es Salaam. Serikali imefuta leseni ya uchapishaji na usambazaji wa Gazeti la Tanzania kutokana na kukiuka sheria za Tanzania na maadili ya vyombo vya habari.
Kuanzia kesho Juni 24, 2020 gazeti hilo halitaruhusiwa kuchapishwa wala kusambazwa popote nchini wala nje ya nchi.
Kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya Habari -Maelezo iliyotolewa leo Juni 23, uamuzi wa kuifuta gazeti hilo mashughuli umefikiwa baada ya jitihada za kulionya gazeti hilo kufuata masharti ya leseni yake kutokuzaa matunda.
“Kwa sababu hizo, kwa mamlaka aliyopewa chini ya kifungu 9 (b) cha Sheria ya Huduma za Habari No. 12 ya mwaka 2016, Mkurugenzi wa Idara ya Habari amefuta leseni ya gazeti hilo ikiwa ni baada ya kulionya zaidi ya mara 10 huku gazeti lenyewe likilazimika kuomba radhi mara mbili kwa uvunjifu wa maadili ya kitaaluma na sheria za nchi ikiwemo kuchapisha habari za uongo, uchochezi na uzandiki,” amesema Patrick Kipangula katika taarifa hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari.
Zinazohusiana:
- LHRC yazungumzia adhabu ya vituo vitatu vya televisheni mtandaoni.
- TCRA yakusudia kusimamisha leseni za DSTV na Zuku.
- CCM yazidi kuongeza umiliki wa vyombo vya habari Tanzania
Aidha, amesema kwa mujibu wa sheria, wachapishaji wa gazeti hilo wanayo fursa ya kuomba leseni upya ikiwa watakuwa tayari kufuata taratibu.
Mbali na kusajili upya gazeti hilo, Kipangula amesema Tanzania Daima lina fursa ya kukata rufaa kwa Waziri wa mwenye dhamana na habari ndani ya siku 30 iwapo hatawaridhika na uamuzi huo.
Tofauti adhabu za miaka ya nyuma kwa gazeti hilo zilizokuwa zinalisimamisha kwa muda, adhabu ya leo inaonekana ni kubwa zaidi kwa kuwa inafuta kabisa leseni hiyo.
Mhariri wa gazeti hilo Martin Malera ameiambia Nukta kuwa barua waliyopokea inaonyesha wamefungiwa kwa “kuchapisha uchochezi, kusambaza habari za uchochezi na zile zisizozingatia maadili.”
Katika barua hiyo, Malera amesema Serikali imeainisha makosa yao yote tangu mwaka 2018 hadi mwaka huu zikiwemo vichwa vya habari vilivyowahi kuleta shida.
“Tunajadiliana na uongozi kuona hatua za kuchukua baada ya kusitishiwa leseni,” amesema Malera akiongeza kuwa barua waliyopokea hivi karibuni kutoka serikalini ilikuwa ikiwataka kujieleza kuhusu habari waliyochapisha kuhusu askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Karagwe, Dk Benson Bagonza.
Latest
