Ethiopia yavunja rekodi ya dunia upandaji miti, Tanzania ikijikongoja
- Yapanda miti zaidi ya milioni 350 kwa saa 12.
- Yavunja rekodi ya dunia iliyoshikiliwa na India tangu mwaka 2016.
- Tanzania bado inapambana na changamoto za kifedha kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Upandaji wa Miti (2016-2021).
Dar es Salaam. Wakati Tanzania ikiendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Upandaji wa Miti wa 2016-2021, nchi ya Ethiopia imevunja rekodi ya dunia ya upandaji miti kwa siku moja baada ya kupanda zaidi ya miti milioni 350 katika bustani ya Gulele katika Jiji la Addis Ababa.
Hiyo ni sawa na kusema kwa saa moja walipanda miti milioni 29.2 huku wakitumia dakika moja kupanda miti milioni 5.8.
Taarifa iliyotolewa na Shirika la mazingira la Umoja wa Mataifa (UN Environment) inaeleza kuwa miti hiyo milioni 350 ilipandwa ndani ya saa 12 na kuvunja rekodi ambayo iliwekwa na India mwaka 2016 ya kupanda miti mingi zaidi kwa siku moja ambayo wakati huo ilikuwa ni miti milioni 50.
Miti hiyo ilipandwa katika uzinduzi wa kampeni ya upandaji miti inayolenga kukabiliana na uharibifu wa misitu na mabadiliko ya tabianchi.
UN Environment inasema kampeni hiyo ni sehemu ya mpango ulioanzishwa na Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed wa kupanda miti na inakusudia kuona kila siku miti milioni 200 inapandwa katika maeneo 1,000 nchini kote.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Ahmed amepongeza Taifa lake siyo tu kukidhi mpango huo lakini pia kuvuka lengo.
Umoja wa Mataifa unakadiria kuwa eneo la misitu Ethiopia limepungua na kufikia asilimia nne katika miaka ya 2000 kutoka asilimia 35 mwanzoni mwa karne ya 20.
Zinazohusiana:
- Teknolojia inavyookoa mazingira
- Wanahabari wahimizwa kuripoti habari za nishati jadidifu.
- Washiriki tamasha la nishati 2018 waondoka na matumaini kibao
Mkurugenzi wa UN Environment Ofisi ya Afrika, Juliette Biao amesema Afrika ina sifa na uwezo wa kusongesha kampeni ya upandaji miti duniani ikizingatiwa kuwa imeathirika zaidi ambapo hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi lazima zipatiwe kipaumbele katika siku zijazo.
“Sisi UN Environment tunaongoza katika kusaidia kujenga uwezo wa mataifa na watu wake kutekeleza wao wenyewe mikakati ya upandaji miti na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,” amesema Biao katika taarifa hiyo.
Kwa rekodi hiyo mpya ya Ethiopia, UN Environment imetaka mataifa mengine ya Afrika yachukue hatua kwa kasi na kuzipatia ufumbuzi changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Kwa mujibu wa chapisho moja katika Jarida la kisayansi, watafiti wanakadiria kuwa upandaji miti kote duniani unaweza kuondoa theluthi mbili ya hewa ukaa inayoingia angani kutokana na shughuli za binadamu ikiwemo viwanda.
Wakati Ethiopia ikivunja rekodi ya dunia, Tanzania bado inaendelea kutekeleza mkakati wake wa upandaji miti huku ikiwa na kibarua kigumu cha kukabiliana na uhaba wa fedha kuhakikisha ifikapo 2021 makakati huo uwe umeleta matokeo katika maeneo mbalimbali nchini.
“Changamoto nyingine ni pamoja na uwasilishwaji wa takwimu zisizo akisi halisi ya upandaji na utunzaji miti katika Halmashauri za Wilaya na upandaji wa miti isiyo rafiki kwa eneo husika,” alisema aliyekuwa Waziri wa Muungano na Mazingira, January Makamba katika hotuba ya bajeti ya wizara yake kwa mwaka 2019/2020.