TMA yazungumzia mvua kubwa zinazonyesha Dar, yatoa tahadhari
- Mvua hizo zimeanza kunyesha leo asubuhi (Desemba 17, 2019) na kusimamisha shughuli za kijamii na kiuchumi.
- Yasema mvua hizo ni matokeo ya kuimarika kwa ukanda wa mvua katika eneo la nchi ya Tanzania.
- Yawataka kuchukua tahadhari ikiwemo kuepuka kukaa chini ya miti na kando ya mito.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema mvua kubwa zinazonyesha leo jijini Dar es Salaam na maeneo mengine ya nchi ni matokeo ya kuimarika kwa ukanda wa mvua na imewataka wananchi kuchukua tahadhari ya kujikinga dhidi ya athari zinazoweza kutokea.
Maeneo mengine kwa mujibu wa TMA ambayo mvua hizo zinanyesha ni pamoja na Dodoma, Singida, Tanga, Pwani, Kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba.
Meneja wa kituo kikuu cha utabiri wa mamlaka hiyo, Samuel Mbuya akizungumzia mvua hizo leo (Desemba 17, 2019) amesema vipindi vya mvua hizo kubwa zitaendelea mpaka leo alasiri baada ya hapo mvua zitapungua na hali itarejea kama kawaida.
“Hali hii inatokana na kuimarika kwa ukanda wa mvua katika eneo la nchi yetu na ukanda huu umesukumwa kaskazini kutokana na mkondo wa baridi katika ncha ya kusini ya bara la Afrika,” amesema Mbuya katika taarifa iliyotolewa na TMA.
Amewataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya athari zinazoweza kutokea ikiwemo kuepuka kukaa chini ya miti na kando ya mito.
MPYA: Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) yawataka wananchi wa jiji la Dar es Salaam na maeneo mengine ya Dodoma, Singida, Kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, Pwani pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba kuchukua tahadhari ya mvua kubwa inayonyesha leo (Desemba 17, 2019). pic.twitter.com/C7ubytL5Pf
— Nukta Tanzania (@NuktaTanzania) December 17, 2019
Mvua hizo ambazo zilianza kunyesha asubuhi hasa katika jiji la Dar es Salaam zimesimamisha shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi ikiwemo usafiri wa magari kutokana na barabara kujaa maji.
Baadhi ya maeneo ya mabondeni yamekumbwa na mafuriko na kuwaletea kadhia wananchi wa maeneo hayo.
Zinazohusiana
- TMA yatoa ushauri, tahadhari ujio mvua za vuli Oktoba
- Kicheko kwa wakulima, TMA akitoa mweleko mvua za msimu
Kutokana na mvua inayoendelea kunyesha jijini Dar es Salaam, Wakala wa Mabasi yaendayo haraka Dar es Salaam (DART) umesitisha kwa muda huduma ya usafiri ya mabasi yake yanayopita barabara ya Jangwani kutoka na mafuriko katika eneo hilo.
Wasafiri wanaotumia mabasi ya DART wameshauriwa kutumia njia mbadala ikiwemo ya Kimara hadi Magomeni Mapipa, Kimara hadi Morocco na Gerezani hadi Muhimbili.
Hata hivyo, wananchi wanashauriwa kuendelea kufuatilia taarifa za utabiri kutoka TMA na kuzingatia tahadhari zilizotolewa na marejeo yake pamoja na kupata na kuzingatia ushauri na miongozo ya wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.
Latest