Famba: Rais Magufuli hajaruhusu daladala kujaza abiria
- Uvaaji barakoa haujakatazwa Tanzania.
- Rais hajaagiza shule zifunguliwe wala madereva kujaza abiria kwenye magari.
- Ikulu imesema Rais hakutoa tamko kama hilo jana Mei 25.
Dar es Salaam. Mitambo ya uzalishaji wa habari za uzushi imeshika kasi baada ya kuzusha tena kuwa Rais John Magufuli ameruhusu daladala kujaza abiria na kupiga marufuku uvaaji wa barakoa ambazo hutumika kujikinga na ugonjwa wa virusi vya Corona.
Tangu jana Mei 24, 2020 zinasambaa taarifa mbili zinazodaiwa kuwa zimetolewa na Dk Magufuli kuhusu hatua ilizochukua Serikali dhidi ya COVID-19 ikiwemo iliyotengenezwa kwenye mtandao wa Twitter.
Taarifa ya kwanza inayodaiwa kutokea kwenye akaunti ya Twitter ya Rais Magufuli inawataka watu kuachana na uvaaji wa barakoa kwa sababu ugonjwa wa Corona umeisha nchini Tanzania jambo ambalo si kweli. 
Tarifa ya pili ikidai imetolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu ikieleza kuwa watu kuandelea kuvaa barakoa ni kuongeza hofu kwenye jamii na kuwa Rais ameagiza shule zifunguliwe na magari hasa daladala zirudi katika utaratibu wa zamani wa kujaza watu.

Nukta Fakti imebaini kuwa taarifa zote hizo mbili ni uzushi mtupu kwa sababu hazijatolewa na mamlaka husika.
Ukweli uko hivi
Ujumbe wa kwanza unaodaiwa kutoka kwenye akaunti ya Twitter ya Rais Magufuli siyo wake na hiyo akaunti ni feki iliyotengenezwa kupotosha umma.
Rais Magufuli Mei 24 hakutoa ujumbe wowote kwa Watanzania, jambo linalothibitisha kuwa taarifa hiyo ni uzushi mtupu.
Sambamba na hilo, katika akaunti rasmi ya Twitter ya Rais Magufuli inaonyesha mara ya mwisho kuweka ujumbe katika ukurasa wake ilikuwa Aprili 16, 2020 ambapo alikuwa akiwahimiza Watanzania kufanya maombi ya siku tatu ili Mungu atuepushe na janga la Corona.
Ndugu zangu Watanzania, kutokana na ugonjwa wa Corona, nawaomba tutumie siku 3 za kuanzia tarehe 17- 19 Aprili, 2020 {Ijumaa, Jumamosi na Jumapili} KUMUOMBA MWENYEZI MUNGU aliye muweza wa yote atuepushe na janga la ugonjwa huu. Tusali kwa kila mmoja kwa imani yake, atatusikia.
— Dr John Magufuli (@MagufuliJP) April 16, 2020
Taarifa ya pili nayo haina ukweli wowote na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu Gerson Msigwa ameutaka umma kuupuza habari kupitia ukurasa wake wa Twitter na kwamba taarifa hiyo haikutolewa na ofisi yake.
Msigwa huwa na kawaida ya kuweka taarifa za Ikulu zinazotolewa kwa umma kupitia akaunti yake ya Twitter lakini kwa siku ya jana hakuweka taarifa kama hiyo zaidi ya kukanusha uzushi huo na video ya Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta.
Lakini ukitazama taarifa hiyo utagundua ina makosa lukuki ya kiuandishi kwa sababu haijapangwa katika mtiririko mzuri na inaonyesha aliyeandika hakuzingatia miiko ya uandishi wa habari au taarifa kwa umma.
Zinazohusiana:
- Ni uzushi mtupu: Wakenya hawajaandamana kupinga zuio la kutotoka nje
- Picha za tetemeko Croatia zilivyotumika kupotosha Corona mtandaoni
- Siyo kweli wananchi Italia wanatupa pesa mitaani kuepuka Corona
Tofauti na taarifa hiyo iliyosema shule zimeruhusiwa kufunguliwa, Mei 21, 2020 Rais aliruhusu kufunguliwa kwa vyuo vyote na wanafunzi wa kidato cha sita pekee ndiyo walioruhusiwa kurudi shule Juni Mosi na siyo ngazi zingine za elimu.
Na kwa upande wa magari kujaza, hakuna tamko lolote la Serikali linalowataka madereva kurudi katika utaratibu wa zamani badala yake daladala zinaendelea kuchukua tahadhari za kutokujaza watu kwenye magari (level seat).
Watanzania wanatakiwa kuendelea kuchukua tahadhari zote ikiwemo kunawa mikono mara kwa mara, kuepuka kugusa macho, pua na mdomo, kuvaa barakoa na kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima.
“Famba, ipuuzwe uendelee kuzingatia ushauri wa wataalamu wetu makini wa afya huku tukijilinda na kuwalinda pia wageni wetu kutoka nchi mbalimbali duniani ambao nasisitiza tena wameanza kumiminika kuja hapa nchini,” amesema Msemaji Mkuu wa Serikali Dk Hassan Abbas katika ukurasa wake wa Twitter. Akielezea taarifa iliyozushiwa Rais Magufuli.