Simu kuuzwa bila chaja, “earphone” ni mapinduzi mapya?
- Baadhi ya kampuni za simu ikiwemo Samsung na Apple zimeanza mipango ya kuanza kuuza simu zake bila kuambatanisha chaja na earphones.
- Watuamiaji wamepokea kwa maoni tofauti hatua hizo huku wengine wakisema itawaongezea gharama za manunuzi.
Dar es Salaam. Utajisikiaje pale umeenda kununua simu mpya dukani na baada ya kufungua boksi lake,unaikuta simu ikiambatana na karatasi za maelekezo pekee?
Yaani, hakuna chaja wala “earphones” kwenye boksi hilo. Ni dhahiri utashangaa na kujiuliza maswali mengi.
Tayari baadhi ya kampuni zinazotengeneza simu zimeanza mchakato wa kutokuambatanisha chaja na earphones wanaposafirisha simu kwenda sokoni.
Moja kati ya simu hizo ni OnePlus 8 ambayo imeingia sokoni hivi karibuni bila earphone, jambo linalowazimu wanunuzi kutumia gharama zingine kupata vifaa hivyo.
“Ninapenda muziki. Siwezi kununua simu ambayo inakuja bila earphones,” amesema Jessica Kimoso mdau wa teknolojia kutoka jijini Dar es Salaam.
Hivi karibuni, kumekuwa na fununu kuwa kampuni ya Apple Inc inayotengeneza vifaa vya kielektroniki nchini Marekani itaitoa simu ya iPhone 12 bila spika zake za masikioni (earbuds) wala chaja.
Hali hiyo huenda ikawaacha nyuma baadhi ya wadau wake wanaopenda kutumia earphones na chaja zinazokuja na simu.
Jessica amesema, mara nyingi anaamini zaidi earphones na chaja zinazokuja na simu ni imara na ndizo zenye kipimo kinachowiana na simu.
Uko tayari kununua simu ambayo haina chaji wala earphone? Picha|Mtandao.
Hata hivyo huenda wadau wa simu hiyo wakasubiri zaidi kwani bado kuna sintofahamu kama simu hiyo itazinduliwa mwaka huu ikiwa Apple ambayo huzindua simu zake mwezi Septemba ni kati ya kampuni zilizoathiriwa kiuzalishaji na janga la corona.
Mbali na OnePlus 8 ambayo imeondoa earphones na kubakiza chaja huenda Samsung pia ikaungana na kampuni hizo mbili kwa baadhi ya simu zake zitakazotoka kuanzia mwaka 2021.
Zinazohusiana
- Samsung, Huawei zinavyochuana katika soko la simu duniani
- Upo tayari kununua simu ya mkononi ya zaidi ya Sh3 milioni?
Kwa mujibu wa taarifa ya iliyotolewa na ETnews, Samsung imeamua hivyo kwasababu inaamini wadau wake tayari wana chaja za simu za Samsung na pia, kupitia njia hiyo, itapunguza gharama za uzalishaji.
Hatua hiyo inaweza pia kupunguza bei ya simu hizo na hivyo kuwapatia ahueni wanunuzi ambao watalazimika kununua vifaa hivyo kukamilisha mawasiliano yao.
Mpiga picha Rahim Mngwaya amesema kwake yeye, yupo tayari kubaki nyuma na kuendelea kutumia simu ambazo zitakuja na bidhaa hizo.
“Bora nihame brand. Sasa ninunue simu peke yake, earphone peke yake na hadi chaja peke yake. Siwezi,” amesema Mngwaya.
Je, wewe utanunua?
Latest