Amazon, Google zashitakiwa matumizi ya picha za watu kwa majaribio
- Ni baada ya kutumia picha za watu bila ridhaa zao katika shughuli za matengenezo ya teknolojia ya utambuzi wa sura (facial recognition).
- Inadaiwa kuwa kampuni hizo zililenga kutumia picha hizo kujinufaisha.Â
Dar es Salaam. Raia wawili nchini Marekani wamezishitaki kampuni za Google, Amazon na Microsoft kwa kutumia picha zao katika matengenzo ya teknolojia ya utambuzi wa uso ya (Facial recognition) bila ridhaa yao.
Raia hao Steven Vance na Tim Janecyk wamefungua kesi katika mahakama za jimbo la California na Washington nchini humo wakidai kampuni hizo zililenga kujinufaisha kwa kutumia picha zao.
Wawili hao ni kati ya sura milioni moja zilizopo kwenye nyaraka za kampuni ya IBM wamesema taarifa zao zimeingizwa kwenye nyaraka hizo bila ridhaa yao na hivyo kuziweka taarifa zao katika sintofahamu.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Cnet, IBM ilikuwa ikifanya maboresho ya teknolojia ya utambuzi wa sura ili teknolojia hiyo isitegemee umri, rangi na jinsia kama ilivyo kwa sasa badala yake itumie picha.Â
Zinazohusiana
- Nukta Africa yateuliwa katika mpango wa Google
- Safari ya mwisho ya Google Plus
- Miaka 15 ya Gmail ilivyongeza thamani bidhaa za Google
IBM ilikusanya picha hizo kutoka kwenye tovuti ya Flickr inayohifadhi maelfu ya picha ambazo zinawekwa kwenye mtandao huo ambapo baadhi zimewekwa pasipo kuwashirikisha wenye picha hizo.
Licha ya kampuni ya IBM kutelekeza utafiti wake mwezi Juni mwaka huu ikihofia teknolojia hiyo kutumika vibaya, nyaraka zake zimetumika na Gooogle, Amazon na Microsoft katika kuendeleza teknolojia hiyo inayohofiwa kusababisha unyanyapaa wa rangi na ukosefu wa haki.
Teknolojia ya utambuzi wa sura imepokelewa kwa maoni tofauti duniani huku baadhi ya watu wakiihusisha na ubaguzi kwani inaonekana kubagua baadhi ya watu wakiwemo waliopo kwenye makundi maalumu.
Teknolojia hiyo inatumiwa katika maeneo mbalimbali zikiwemo maduka makubwa na viwanja vya ndege ili kuimarisha usalama wa watu.