Hapana: Kuosha pua kwa maji ya chumvi hakuzuii Corona
- Virusi vya ugonjwa wa Corona haviwezi kudhibitiwa kwa kuosha pua kwa maji yenye chumvi.
- Njia ya kujikinga na COVID-19 ni pamoja na kunawa mikono, kuvaa barakoa na kutumia kitakasa mikono.
Dar Es Salaam. Wakati wataalam wa afya wakiendelea na mapambano dhidi ya janga la Corona (COVID-19), bado habari za uzushi kuhusu ugonjwa huo zinaendelea kusambaa kwa kasi duniani.
Miongoni mwa habari hizo za uzushi zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii, ni zile zinazodai kuwa kuosha pua mara kwa mara kwa kutumia maji yenye chumvi ni njia mojawapo ya kumkinga mtu na maambukizi ya Corona
Hata hivyo, taarifa hizo hazina ukweli wowote, ni uongo ambao unalenga kuwapotosha watu.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema virusi aina ya COVID-19 haviwezi kudhibitiwa kwa kuosha pua kwa maji yenye chumvi.
“Hakuna ushahidi unaothibitisha kuwa kuosha pua mara kwa mara kunaweza kumkinga mtu dhidi ya maambukizi ya Corona,” imesema WHO.
WHO inasisitiza kuwa njia pekee ya kujikinga na COVID-19 ni kunawa mikono mara kwa mara kwa maji tiririka na sabuni; kutumia tishu wakati wa kukohoa au kupiga chafya; kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima na kuvaa barakoa.