Rais Magufuli afuta sherehe za Uhuru kwa mara ya tatu

December 3, 2020 1:08 pm · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Sherehe hizo zilitakiwa kufanyika Desemba 9, 2020.
  • Aagiza fedha za sherehe zitumike kununua vifaa vya hospitali ya Uhuru mkoani Dodoma. 
  • Hii ni mara ya tatu kwa Rais kufuta sherehe za uhuru. 

Dar es Salaam. Rais John Magufuli ameahirisha maadhimisho ya sherehe za Uhuru wa Tanzania Bara zilizotarajiwa kufanyika Desemba 9, 2020 na ameelekeza fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kufanikisha sherehe hizo zitumike kununulia vifaa mbalimbali kwa ajili ya hospitali ya Uhuru ya mkoani Dodoma. 

 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa katika taarifa yake iliyotolewa leo Desemba 3, 2020 amesema Dk Magufuli ameagiza Sh835.5 milioni zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kufanikisha sherehe hizo zitumike kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya hospitali hiyo.

Majaliwa aliyekua akizungumza wakati wa sherehe za kuadhimisha miaka 60 ya kuanzishwa kwa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) jijini Dar es Salaam amesema siku hiyo itatumika kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali za kijamii. 

Hii ni mara ya tatu kwa Rais Magufuli kuahirisha sherehe za uhuru ambapo awali alifanya hivyo Desemba 2015 mwezi mmoja tu tangu aingie madarakani.

Fedha zilizotengwa aliagiza zitumike kupanua kipande cha barabara kutoka Morocco hadi Mwenge Jijini Dar es Salaam.

Pia alifanya hivyo tena mwaka, 2018 ambapo aliagiza aliagiza kiasi cha Sh995.2 milioni zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya maadhimisho ya 57 ya sherehe hizo zitumike kujenga hospitali ya Uhuru, ambayo kwa sasa ujenzi wake umefikia asilimia 92.


Zinazohusiana:


Majaliwa amesema hadi kufikia sasa ujenzi wa hospitali hiyo ya Uhuru umegharimu Sh4.2 bilioni. 

Hospitali hiyo itakayojengwa katika eneo la kati ya barabara ya kwenda Hombolo na Chamwino kwenye barabara ya kwenda Dar es Salaam itakuwa inawahudumia wakazi wa mkoa wa Dodoma pamoja na mikoa ya jirani.

Kauli mbiu ya maadhimisho ya 59 ya Uhuru wa Tanzania Bara kwa mwaka huu inasema; ‘Miaka 59 ya Uhuru na Miaka 58 ya Jamhuri: Tanzania yenye Uchumi Imara Itajengwa na Watanzania Wenyewe, Tufanye Kazi kwa Bidii, Uwajibikaji na Uadilifu.’

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW